Jumamosi, Julai 12, 2014

BRAZIL YAZIDI KUTAWALIWA NA SIMANZI

Majonzi ya wenyeji wa Kombe la Dunia, Brazil yalizidi baada ya Uholanzi kuwacharaza 3-0 kwenye mechi ya kuamua nafasi ya tatu jijini Brasilia Jumamosi usiku.
Huku wakiendelea kuomboleza kuchabangwa 7-1 na Ujerumani katika nusu fainali, Brazil walijipata mashakani zaidi dakika tatu pekee baada ya kipenga cha mwanzo wakati Robin van Persie alipopachika wavuni penalti na hivyo kuwapa Uholanzi uongozi. Daley Blind alifaidika kutoka kosa la beki David Luiz dakika zilipokatika 17 kuongezea chumvi kwenye kidonda cha wenyeji ambao walikuwa na nyota wao maarufu aliyejeruhiwa, Neymar, akitizama kutoka benchi. Georginio Wijnaldum alikamilisha fedheha ya Wabrazil katika muda wa ziada kwa bao la tatu na hivyo kuzidisha gadhabu kutoka mashabiki ambao walichukizwa na kusambaratika kwa mabingwa hao wa mara tano wa Kombe la Dunia. Brazil walipoteza mechi mbili mtawalia nyumbani kwa mara ya kwanza tangu 1940 na walimaliza shindano hili wakiwa wamepokea mabao 14 ambayo ni mengi zaidi kwa timu zinazoshiriki Kombe la Dunia tangu 1986. Uholanzi wameuchukua nafasi ya tatu na kumaliza shindano hili bila kuonja kichapo baada ya kuondolewa semi fainali kupitia mikwaju ya penalti. Walipoteza kiungo wao tegemeo, Wesley Sneijder, ambaye alilazimishwa kukosa mechi hiyo baada ya kupata jeraha dakika chache kabla ya mechi hiyo kuanza huku Jonathan de Guzman akidhibiti nafasi yake.

0 comments:

Chapisha Maoni