Alhamisi, Machi 27, 2014

SASA VITA IMETANGAZWA JAMHURI YA AFRIKA YA KATI

Kikosi cha kusimamia amani cha Umoja wa Afrika MISCA kilichoko katika Jamhuri ya Afrika ya Kati kimetangaza vita dhidi ya wanamgambo wa Kikristo wa Anti-Balaka ambao wamekuwa wakiwauwa kinyama Waislamu wa nchi hiyo.
Hatua hiyo ni radiamali ya vikosi hivyo baada ya askari wake kushambuliwa na wanamgambo hao. Jenerali Jean Marie Michel Mokoko, kamanda wa kikosi cha MISCA katika Jamhuri ya Afrika ya Kati ametangaza kuwa, kuanzia sasa wanawahesabu wanamgambo wa Anti Balaka kuwa ni maadui wao na watahakikisha wanakabiliana nao vilivyo. Kikosi hicho cha Umoja wa Afrika kimekuwa kikipambana na wanamgambo wa Anti-Balaka katika mji mkuu Bangui tangu siku ya Jumamosi ambapo kwa uchache watu 16 wanaripotiwa kuuawa katika mapigano ya hivi karibuni kabisa nchini humo. Wakati huo huo, Shirika la Msamaha Duniani la Amnesty International limetoa wito wa kutumwa kikosi cha kusimamia amani cha Umoja wa Ulaya huko Jamhuri ya Afrika ya Kati. Taarifa ya Amnesty International imebainisha kwamba, hali ya mambo katika Jamhuri ya Afrika ya Kati inatia wasi wasi kwani wanamgambo wa Anti-Balaka kila siku wamekuwa wakidhibiti maeneo zaidi katika mji mkuu Bangui na kuendelea kufanya mauaji.

0 comments:

Chapisha Maoni