Alhamisi, Mei 15, 2014

WANANCHI WA WILAYA YA KYELA-MBEYA KATIKA MAZINGIRA HATARISHI

ZAIDI ya Wananchi 100,000 wilayani Kyela mkoani Mbeya wapo hatarini kukumbwa na magonjwa ya mlipuko kutokana na kutumia maji yasiyofaa kwa afya za binadamu kufuatia visima vyao vya awali kuharibiwa na mafuriko yaliyotokea wilayani humo April 12 mwaka huu.
Hatari hiyo inatokana na wananchi hao sasa kulazimika kutumia maji yaliyotuama kwenye maeneo yao baada ya kutokea kwa mafuriko hayo kwa ajili ya kunywa na kupikia vyakula
Mkuu wa Wilaya ya Kyela, Margret-Esther Malenga, amesema kati ya kata 20 zilizomo wilayani humo, kata 12 wananchi wake bado wamezingirwa na maji hivyo wanalazimika kutumia maji yasiyo salama kwa ajili ya kujikimu kwa maisha yao ya kila siku.  
 Malenga ametoa taarifa hiyo wilayani humo wakati akipokea msaada ya dawa za binadamu kutoka kwa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, NHIF, ili kukabiliana na magonjwa yatakayotokana na mafuriko hayo.
Wilaya ya Kyela ina zaidi ya wakazi 225,000, Malenga, amesema takwimu zinaonesha kuwa zaidi ya nusu ya wakazi hao wanakabiliwa na hatari ya kukumbwa na magonjwa ya mlipuko kutokana na kutumia maji hayo.
Kibaya zaidi, Malenga amesema licha ya Wataalam wa wilaya hiyo kuwaelimisha wananchi hao kuchemsha maji hayo ili kujiepusha na magonjwa lakini bado wanakabiliwa na wakati mgumu wa kutekeleza ushauri huo kutokana na kwamba hakuna kuni za uhakika kufuatia miti yote kubaki majini.
Mganga Mkuu wa Wilaya hiyo, Festo Dugange amesema tayari wameanza kuchukua tahadhari ya kuhakikisha wanakuwa na dawa za kutosha endapo mlipuko huo wa magonjwa utajitokeza pamoja na kutoa elimu kwa wananchi hao kuhusu umuhimu wa kuchemsha maji ya kunywa.
Meneja wa NHIF Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Mohammed Kilolile, amesema mfuko huo utaendelea keshirikiana na Serikali wilayani humo ili kuhakikisha uthibiti wa kutosha wa magonjwa hayo endapo yatatokea.
Jumla ya kaya 3,983 zimeathiriwa na mafuriko hayo wilayani Kyela na kusababisha watu kadhaa kukosa makazi.

0 comments:

Chapisha Maoni