Ijumaa, Mei 16, 2014

UGOMVI WA NG'OMBE SHAMBANI WAUA MTU MBEYA

Fred Mwakibinga [55], mkazi wa kijiji cha Kanga – Ipinda wilaya ya Kyela alifariki dunia akiwa njiani kupelekwa hospitali baada ya kushambuliwa kwa kupigwa ngumi na mateke mwilini na Karume Sokoni [35], mkazi wa kijiji cha Kanga.
Tukio hilo limetokea tarehe 14.05.2014 majira ya saa saba mchana huko katika kijiji cha Kanga, kata ya Ipinda, tarafa ya Ntebela wilaya ya Kyela. Chanzo cha tukio ni ugomvi uliotokea kati ya marehemu na mtuhumiwa baada ya mtuhumiwa kufunga ng’ombe wake kwenye shamba la marehemu bila idhini yake na marehemu kutaka kuzitoa ng’ombe hizo siku ya tarehe 11.05.2014 majira ya saa 6 mchana, hivyo marehemu aliendelea kupata matibabu akiwa nyumbani hadi hali ilipobadilika. Mtuhumiwa alikimbia mara baada ya tukio hilo.
Kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya kamishina msaidizi mwandamizi wa polisi Ahmed Msangi anatoa wito kwa jamii kujenga tabia ya kutatua migogoro yao kwa njia ya kukaa meza ya mazungumzo ili kuepuka matatizo yanayoweza kuepukika.aidha anatoa rai kwa yeyote mwenye taarifa juu ya mahali alipo mtuhumiwa azitoe katika mamlaka husika ili akamatwe na sheria ichukue mkondo wake.

0 comments:

Chapisha Maoni