Jumatatu, Aprili 03, 2017

UMASIKINI KUONGEZEKA MAREKANI

Taasisi ya utafiti ya Gallup yenye makao yake makuu mjini Washington Marekani imetangaza habari ya kuongezeka idadi ya wananchi wa nchi hiyo walio na wasiwasi wa kupanda kiwango cha ukata hasa kati ya watu wa pato la chini na tabaka la watu masikini nchini humo.

Uchunguzi wa maoni uliofanywa na taasisi hiyo kuanzia tarehe mosi hadi tarehe tano mwezi uliopita wa Machi unaonesha kuwa, karibu asilimia 67 ya Wamarekani wenye kipato cha chini wana wasiwasi mkubwa wa kukumbwa na umaskini mkubwa zaidi na kupoteza makazi yao. Uchunguzi huo unaonesha kuweko ongezeko kubwa la Wamarekani wenye wasiwasi wa kukumbwa na matatizo hayo ikilinganishwa na miaka ya 2010 na 2011.
Uchunguzi wa huko nyuma wa maoni ulionesha kuwa asilimia 51 ya raia wa Marekani walikuwa na wasiwasi wa kuongezeka umaskini na kupoteza makazi yao.
Utafiti wa shirika la Gallup uliofanywa mwaka 2014 nchini Marekani ulionesha kuwa idadi ya Wamarekani waliokuwa na wasiwasi wa kupoteza makazi yao na kuongezeka umaskini wao haikupindukia asilimia 35 wakati huo.
Machafuko, vitendo vya utumiaji mabavu, uhalifu, jinai na ukosefu wa amani na usalama ni mambo mengine yanayozifanya nyoyo za wananchi wa Marekani kuwa na wasiwasi mkubwa hususan kati ya matabaka ya watu maskini na wenye kipato cha chini.
Matokeo ya uchunguzi wa hivi sasa wa taasisi ya Gallup unaonesha kuwa Wamarekani wa matabaka yote wana wasiwasi wa kupoteza makazi yao na kuongezeka umaskini na kwamba idadi yao imeongezeka sana hivi sasa ikilinganishwa na miaka ya huko nyuma.

0 comments:

Chapisha Maoni