Jumapili, Aprili 02, 2017

PAPA FRANCIS ATAKA KUIMARISHWA AMANI DRC

Kiongozi wa Kanisa Katoliki Duniani Papa Francis ametoa wito wa kuimarishwa amani na utulivu katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo akitilia mkazo suala la kukomeshwa umwagaji damu katika mkoa uliozongwa na machafuko wa Kasai.
Papa Francis amesema kuwa, kunaendelea kutolewa ripoti na habari za mapigano ya umwagaji damu katika eneo la Kasai huko Congo DR ambayo yanawaathiri raia na kuwalazimisha wengine kuwa wakimbizi.
Kiongozi wa Kanisa Katoliki amewataka wanadamu kuomba dua ya amani na kuwaombea wale wanaofanya jinai na mauaji hayo kuondoka katika utumwa wa chuki na ukatili.
Watu wasiopungua 400 wameuawa katika machafuko yanayoendelea kwa miezi kadhaa sasa katika mkoa wa Kasai ulioko katikati mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo. 
Mkoa wa Kasai umekumbwa na ghasia tangu katikati ya mwezi Agosti, wakati askari wa kikosi cha serikali ya Congo walipomuua Kamwina Nsapu, aliyekuwa kiongozi wa wanamgambo waasi dhidi serikali kuu Rais Joseph Kabila.
Wakati huo huo Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC) imetahadharisha kuwa ukatili unaofanyika katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ikiwa ni pamoja na mauaji ya wataalamu wawili wa Umoja wa Mataifa unaweza kutambuliwa kuwa ni jinai ya kivita. 
Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Mahakama ya Kimataifa ya Jinai Fatou Bensouda amesema kuwa hatasita kuwachukulia hatua na kuwapandisha kizimbani watu wanaohusika na uhalifu huo.

0 comments:

Chapisha Maoni