Jumanne, Machi 21, 2017

VIDEO ZA MAUAJI DRC ZAZUA KIZAAZAA

Kutolewa kwa mikanda zaidi ya video za mauaji yaliyofanywa na jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo dhidi ya raia wa nchi hiyo kumeingiza kashfa hiyo katika awamu mpya.
Mikanda hiyo ya video ya mauaji ya raia iliyoonyeshwa katika mitanda ya kijamii, imetoa changamoto kubwa kwa serikali ya Kinshasa. 
Mikanda hiyo inawaonesha wanajeshi wa serikali ya Congo wakiwaua kikatili raia wanachama wa kundi la Kamuina Nsapu katika mkoa wa Kasai. Mmoja kati ya mikanda hiyo ya video ambao ulichukuliwa mwezi Januari mwaka huu unaonesha picha za kaburi la umati lililogunduliwa eneo al Kasai. 
Awali serikali ya Congo ilidai kuwa filamu hizo ni za kubuni lakini baadaye mahakama ya nchi hiyo ilianza kushughulikia watu waliohusika na mauaji ya raia hao. 
Hadi sasa watu saba wametiwa nguvuni kwa tuhuma za kutenda jinai dhidi ya binadamu, kuua na kukata viungo vya miili ya binadamu. 
Umoja wa Mataifa imetangaza kuwa, jeshi la serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo liliua wanachama 101 wa kundi la Kamuina Nsapu katika jimbo la Kasai mwezi uliopita wa Februari. 
Wahanga wengi wa mauaji hayo ni watoto na vijana waliopigwa risasi. Mahakama ya Congo DR imetangaza kwamba inafanya uchunguzi zaidi kuhusu mauaji hayo.

0 comments:

Chapisha Maoni