Jumatatu, Julai 14, 2014

CHANGAMOTO YA TIMU MPYA KATIKA LIGI KUU

TIMU ngeni katika Ligi Kuu ya msimu ujao ambao utaanza Septemba 20, ni Ndanda FC ya Mtwara, Polisi ya Morogoro na Stand United ya Shinyanga zikiziba nafasi ya zilizoshuka ambazo ni Ashanti Utd, JKT Iljoro na Rhino ya Tabora.
Wakati timu zote zikijianda kwa ligi hiyo, timu ngeni zinapaswa kuiga ari ya timu ya Mbeya City iliyoingia Ligi Kuu kwa mara ya kwanza msimu uliopita na kutwaa nafasi ya tatu, ikitanguliwa.

Kama timu ya Mbeya City imeweza kuzichachafya timu kongwe na kuwa tishio, kwa nini timu za Ndanda FC, Stand United na Polisi ya Morogoro zisiweze? Timu zinazoshiriki Ligi Kuu ya Vodacom hakuna yenye hakimiliki ya kutwaa ubingwa mara zote kwani mashindano ni tendo la kupimana uwezo katika jambo. Ni makabiliano yenye lengo la kuwania jambo baina ya pande mbili au zaidi. Mwenye bidii ndiye anayeibuka mshindi.
Timu hizo zisiogope majina yaliyozoeleka ya wachezaji kwani wote wana miguu miwili na kuingiza wachezaji 11 uwanjani kama wao. Kadhalika wasihofie umaarufu wa vilabu kwani navyo pia vilianza kama vyao. Madhali wamejumuishwa na timu kongwe zenye uzoefu, nazo zijione kuwa sawa kwani zimewekwa pamoja kuwania ubingwa utakaopatikana kwa ushindi dhidi ya zingine. Katika michezo kuna waamuzi wanaosimamia haki.
Nazikumbusha kungali mapema kuwa “mwenye kisu kikali ndiye alaye nyama. Anayekishika kisu kikali ndiye anayeweza kuikata nyama vizuri. Methali hii yatukumbusha kuwa aliyejiandaa vizuri ndiye awezaye kufanikiwa katika jambo fulani. Nawashauri wajiandae ipasavyo kabla ya kuliingilia jambo. Kwa kuwa Ligi Kuu iliyokuwa ianze Agosti 28 mwaka huu imesogezwa mpaka Septemba 20 kupisha michuano ya Klabu Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati itakayoanza Agosti 8 na kumalizika Agosti 24 nchini Rwanda, ni kama nafuu ya mchukuzi kwa timu hizo kuwa na muda zaidi wa kujiandaa.

0 comments:

Chapisha Maoni