Jumamosi, Julai 12, 2014

ADA ZA SHULE/VYUO ZAPINGWA

Wakati Serikali ikiendelea kutafuta ‘mwarobaini’ wa kushuka kwa elimu, wadau mbalimbali wameitaka kuachana na mpango wa kupanga bei elekezi kwenye ada za shule na vyuo nchini kwa kuwa hilo siyo suluhisho.
Wakizungumza wakati wa uzinduzi wa ripoti iliyochunguza hali ya sheria na sera za ushindani wa kibiashara nchini, washiriki hao walisema baadhi ya viongozi wakiwamo wabunge wamekuwa wakipendekeza shule na vyuo vyote nchini kutoza viwango sawa vya ada, bila kuzingatia tofauti za kipato kwa wananchi.
Akizungumza katika mkutano  uliofanyika hivi karibuni jijini hapa, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Kupunguza Umaskini (REPOA), Profesa Samuel Wangwe alisema elimu haipaswi kuwekewa kikomo cha ada, badala yake zitafutwe sababu zilizoshusha hadhi ya taasisi hiyo.
Elimu siyo bidhaa unayoweza kuipangia bei, kama mtu anaweza kumlipia mtoto ada Sh4 milioni alipe, kwa sababu wapo watu wanaowalipa watoto wao ada Ulaya Sh20 milioni.
alisema Wangwe.
Alisema shule za sekondari za umma ikiwamo Pugu zilikuwa zikitegemewa kwa kufaulisha wanafunzi, lakini hivi karibuni zimekuwa zikifanya vibaya kitaaluma. Hivyo ni vyema serikali ikatafuta sababu za matokeo mabaya, badala ya kushughulikia viwango vya ada pekee yake.
Kama shule za umma zinafanya vizuri hata hao wanaoweka ada ya Sh4 milioni watapunguza tu.
aliongeza.
Mwakilishi kutoka Tume ya Ushindani (FCC), Shadrack Nkelebe, alisema wadau wa elimu wanapaswa kuwekewa mazingira mazuri ya ushindani yatakayowawezesha kuboresha taasisi hiyo na kuwanufaisha walaji kwa kuongeza ubora wa elimu.
Alisema hivi sasa dunia inaondokana na upangaji wa bei katika biashara ili kuwaongezea wafanyabiashara uwanja wa kushindana kwa uhuru na kwa kufuata sheria.
Udhibiti wa shule unaweza kupunguza ubora wa elimu, acha kupunguza ada kwa matajiri na kuongeza kwa maskini.
alisema Nkelebe.
Akiwasilisha matokeo ya utafiti huo uliofanyika Dar es Salaam pekee, Dk Halima Noor kutoka REPOA, alisema ripoti hiyo imebaini mambo kadhaa yanayowakera wananchi, ingawa asilimia 52 ya watu waliohojiwa walisema hawaijui taasisi yoyote inayoshughulikia ushindani wa kibiashara nchini.
Ripoti hiyo imebaini kuwa wananchi wanaamini kwamba baadhi ya kampuni zinapanga bei ya bidhaa zake kwa lengo la ‘kuwaumiza’ wateja, jambo lililo kinyume na sheria ya ushindani katika biashara.
Asilimia 48 walisema kampuni zinapanga bei za bidhaa kinyume cha sheria, wengine walisema ingawa sekta ya usafiri Dar es Salaam ina ushindani mkubwa, gharama ya nauli ipo juu.
alisema Dk Halima.

0 comments:

Chapisha Maoni