Jumapili, Januari 19, 2014

UJENZI WA SOKO LA KIMATAIFA LA MWANJERWA MBEYA KUENDELEA

Ujenzi wa Soko la Mwanjelwa la jijini hapa ambao ulisimama kwa karibu mwaka mzima unatarajiwa kuendelea tena mapema mwezi ujao kama jiji litafanikiwa kupata mkopo mwingine kutoka Benki ya CRDB.

Mipango ya kupata mkopo wa Sh3.48 bilioni kuamuliwa Januari 23, mwaka huu
Meya wa Jiji la Mbeya, Athanas Kapunga aliwaambia waandishi wa habari kwamba ujenzi huo utaanza kwa kumtumia mkandarasi mpya wa ujenzi anayeitwa Nandhra Engineering and Construction Company Limited ambaye atafanya kazi hiyo kwa gharama ya Sh5.3 bilioni.
Kapunga alisema kazi hiyo itatarajiwa kukamilika chini ya miezi minane na kwamba mkandarasi huyo ametoa uhakikisho wa kukamilisha kazi hiyo ikiwa mambo yatakwenda kama ilivyopangwa.
Hata hivyo, Kapunga alisema kuanza kwa kazi hiyo kutategemea kukamilika kwa mipango ya kutaka kukopa zaidi ya Sh3.48 bilioni kwenye Benki ya CRDB ambayo bodi yake itakaa Januari 23 baada ya jiji kuwasilisha nyaraka zote muhimu kwenye benki hiyo.
Akizungumzia utata na kukwama kwa ujenzi wa soko hilo ambao ulianza Februari 25, 2010, Kapunga alisema mkandarasi mjenzi Tanzania Building Works Company Limited alikwama kukamilisha ujenzi na aliamua kuondoka eneo la ujenzi kutokana na matatizo anayoyajua yeye.
Alisema ujenzi huo ulikuwa ukifanywa kwa gharama ya Sh 13 biloni ambazo zilikopwa Benki ya CRDB na ulitarajiwa kumalizika Agosti 25,2011.
“Ujenzi hadi ulipofikia uligharimu zaidi ya Sh10.2 bilioni na salio la fedha zilikuwa Sh1.81 bilioni, lakini kwa bahati mbaya riba nayo imekuwa Sh1.56 bilioni’’ alisema.
Kapunga alisema pamoja na utata huo, Benki ya CRDB imeonyesha nia ya kutaka kutoa mkopo mwingine ili umalizie kazi hiyo wakati Jiji nalo linalipa madeni pamoja na riba katika kipindi maalumu.

0 comments:

Chapisha Maoni