Alhamisi, Januari 23, 2014

MHOLANZI HANS VAN DER PLUIJM ATAMBA KUIPAISHHA YANGA

Kocha wa Yanga, Mholanzi Hans van der Pluijm amesema uzoefu wake wa miaka 15 kufundisha soka barani Afrika utasaidia kuipa mafanikio Yanga katika mashindano ya Klabu Bingwa Afrika yanayoanza mapema mwezi ujao.
Akizungumza na Fichuo kwa njia ya mtandao akiwa Uturuki jana
, Kaimu Ofisa Habari wa Yanga, Baraka Kizuguto alisema kocha huyo alibainisha hayo mara tu baada ya mazoezi ya jana asubuhi.
“Nina uzoefu na soka la Afrika kwa takribani miaka 15, wachezaji niliowakuta hapa (Yanga) wote wana uwezo mzuri, wanajituma, wana nidhamu na upendo wa hali ya juu, mwalimu yoyote lazima atafurahia kwa kuwa mazingira ya ufanyaji kazi yanakuwa mazuri,” alisema Kizuguto akimnuku kocha huyo.
Kizuguto alisema Kikosi cha Yanga, ambacho kimepata pigo baada ya kuzuiwa kwa usajili wa mshambuliaji wake hatari Mganda Emmanuel Okwi, kiliendelea na mazoezi ya mwisho jana jioni na leo mchana kuanza kwa safari ya kurejea Tanzania.

Aidha, ofisa huyo alisema kuwa Pluijm amesema kambi yao ya wiki mbili kwenye mji unaotajwa kuwa wa matanuzi wa Antalya, Uturuki imekuwa na manufaa makubwa katika kuimarisha kikosi na anaamini timu yake ipo tayari kutetea ubingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom na kufanya vizuri kimataifa.
“Hakuna majeruhi na wachezaji wanajituma na kuwajibika kwa kujua wajibu wao. Tunashukuru Mungu kambi yetu ya siku 14 katika Hoteli ya Sueno Beach Side, Manavgat jijini Antalya inakwenda vizuri,” alisema Kizuguto.
Yanga ilikuwa imeweka kambi nchini Uturuki kwa wiki mbili kama ilivyofanya mwaka jana, ikicheza michezo minne ya kirafiki dhidi ya timu za Ankara Sekerspor (ilishinda 3-0) na Altay SK (ilishinda 2-0) za Ligi Daraja la pili nchini humo kabla ya kuivaa timu ya KS Flumartari ya Albania (0-0) kisha kumaliza na timu ya Simurq PIK ya Azerbajain (2-2).
Vinara hao wa msimamo wa Ligi Kuu Bara watacheza mchezo wao wa kwanza mzunguko wa pili dhidi ya Ashanti United kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam keshokutwa.

0 comments:

Chapisha Maoni