Alhamisi, Desemba 12, 2013

SYRIA BADO HAPAKALIKI

Wizara ya Mambo ya Nje ya Syria imeandika barua kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa na kwa Rais wa Baraza la Usalama la umoja huo ikiwataka wachukue hatua za kukabiliana na uungaji mkono na utoaji misaada unaofanywa na Saudi Arabia kwa makundi ya takfiri na ya kigaidi nchini humo. Katika barua hizo imeelezwa kuwa kauli ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Saudia kwamba nchi yake inajivunia na kuona fahari kuwa inatuma silaha na kupeleka magaidi huko Syria ni jambo la hatari na kwamba kuna ulazima wa kuchukuliwa hatua kali dhidi ya serikali ya Riyadh.
Serikali ya Syria imeshaandika barua kadhaa kwa jumuiya za kimataifa kuhusiana na harakati chafu zinazoendeshwa na madola ya kigeni ndani ya nchi hiyo lakini hadi sasa haijapata jibu lolote la maana. Hivi sasa pia ambapo Lakhdhar Brahimi, mjumbe wa pamoja wa Umoja wa Mataifa na Jumuiya ya Nchi za Kiarabu katika mgogoro wa Syria yuko katika hekaheka za kukamilisha maandalizi ya mkutano wa Geneva 2 ambao ajenda yake kuu ni kuutafutia ufumbuzi wa kisiasa mgogoro huo, baadhi ya nchi kama Saudi Arabia zingali zinaendelea kufanya uafriti ili kukwamisha juhudi hizo na wakati huohuo kukoleza moto wa mgogoro nchini Syria.

Kuna ushahidi na nyaraka chungu nzima zinazoonyesha kuwa serikali ya Saudia imekuwa ikiwaachia huru wafungwa sugu walioko kwenye jela za nchi hiyo na kuwapeleka huko Syria kupigana vita dhidi ya serikali ya nchi hiyo. Hatua kama hiyo inaweza kuwa na maana nyengine ghairi ya kupalilia mbegu za fitina na kukoleza moto wa mgogoro nchini Syria?
Kwa muda wote huu, msimamo wa utawala wa kifalme wa Aal Saud kuhusiana na mgogoro wa Syria umekuwa ni wa kuyasaidia kwa hali na mali makundi ya kigaidi yanayofanya hujuma ndani ya ardhi ya nchi hiyo. Baadhi ya viongozi wa Syria wameutafsiri msimamo huo wa Saudia kuwa ni sawa na kuuhalalisha kisheria ugaidi nchini Syria na ambao ndio ukweli wa mambo. Katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita Saudi Arabia imekuwa mmoja wa wadhamini wakuu wa misaada ya fedha na silaha kwa waasi na magaidi walioko nchini Syria, na katika hili haiwezi kufumbiwa macho nafasi ya Bandar bin Sultan, mkuu wa vyombo vya intelijinsia na vya usalama vya Saudia katika kuyaimarisha magenge ya kigaidi nchini Syria. Aidha kuna taarifa nyingi zinazoonyesha kuwa shirika la intelijinsia la Saudia, kwa kushirikiana na baadhi ya nchi jirani na Syria ikiwemo Uturuki na Jordan, linawatuma huko nchini Syria magaidi waliopewa mafunzo maalumu. Kwa msingi huo hakuna shaka inayosalia kwamba kuibuka mgogoro nchini Syria na kuendelea kwake ni matokeo ya mashirikiano ya waziwazi kati ya Marekani na waitifaki wake wa eneo hususan Saudi Arabia, Qatar na Umoja wa Falme za Kiarabu, Imarati.
Wizara ya Mambo ya Nje ya Syria imetangaza kuwa asilimia 10 hadi 15 ya magaidi wanaofanya vitendo vya ukatili na umwagaji damu nchini humo ni raia wa Saudi Arabia. Magaidi hao wanaingizwa katika makundi kama vile Dola la Kiislamu la Iraq na Sham, Harakati ya An Nusrah na magenge mengine ya kigaidi likiwemo la Abdullah Azzam, ambayo yote hayo yanafuata miongozo ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja kutoka kwa madola ya Magharibi na Saudi Arabia.  Nukta ya kuzingatiwa hapa ni kwamba makundi hayo ya kigaidi yanatenda kila aina ya jinai nchini Syria bila ya hofu wala kujali chochote. Kwa maelezo haya hakuna chembe ya shaka inayosalia kwamba Syria imekuwa mhanga wa njama inayotekelezwa kwa ushirikiano wa kambi mbili za Magharibi na ile ya Kiarabu, njama ambayo moto wake utakuja kuzitambalia pia nchi za Kiarabu zinazofuata sera za Magharibi na Marekani dhidi ya nchi hiyo

0 comments:

Chapisha Maoni