Rais Jacob Zuma wa Afrika Kusini, Alhamisi usiku
alitangaza kifo cha rais wa kwanza mweusi nchini humo, Nelson Mandela,
ambaye amefariki dunia tarehe 5 Desemba 2013 akiwa na umri wa miaka 95.
Rais Zuma anasema, "Mpendwa wetu Nelson
Rolihlahla Mandela, mwasisi wa taifa letu la kidemokrasia, ameaga dunia.
Ameondoka kwa amani akiwa na familia yake saa mbili na dakika 50 usiku
kwa saa za Afrika Kusini, tarehe 5 Desemba 2013. Kwa sasa anapumzika.
Kwa sasa ana amani.
"Taifa
letu limempoteza mtoto wake mkuu wa kiume. Watu wetu wamempoteza baba.
Licha ya kwamba tulifahamu kuwa siku kama hii ingemtokea, hakuna
kinachopunguza upendo wetu kwake na hasara kubwa tuliyopata. Jitihada
zake kutafuta uhuru zimemjengea heshima kubwa duniani.
"Unyenyekevu wake, upendo wake na utu wake,
vimesababisha watu kumpenda. Mawazo yetu na sala zetu tunazielekeza kwa
familia ya Mandela. Kwao tuna deni kubwa la kuwashukuru. Walijitolea kwa
kiasi kikubwa na kuvumilia mengi ili watu wetu wawe huru. Amesema Zuma.
"Mawazo yetu yapo pamoja na mkewe Graça Machel,
mke wake wa zamani Winnie Madikizela-Mandela, pamoja na watoto wake ,
wajukuu wake na familia nzima. Mawazo yetu yapo pamoja na rafiki zake,
marafiki katika mapambano na washirika wake walioshirikiana na Madiba
katika mapambano ya ukombozi.
"Mawazo yetu yapo pamoja na wananchi wa Afrika
Kusini ambao leo wanaomboleza kifo cha mtu,ambaye zaidi ya wengine
amekuja kuleta hisia ya taifa moja. Mawazo yetu yapo pamoja na watu
duniani kote ambao wamemkubatia Madiba kama mtu wao, na ambaye aliona
matatizo yao ni yake.



0 comments:
Chapisha Maoni