Ijumaa, Novemba 08, 2013

BUNGE LIMEFANYA MABADILIKO YA KALENDA YAKE

Bunge limefanya mabadiliko makubwa katika kalenda ya mikutano yake ili kutoa fursa kwa Bunge Maalumu la Katiba lililopangwa kufanyika kati ya Januari na Machi 2014.
Kamati ya Uongozi ya Bunge iliyokutana Jumatano wiki hii chini ya uongozi wa Spika Anne Makinda ilifanya mabadiliko ya mkutano wa 14 ambao sasa utaanza Desemba 3 na kuendelea kwa wiki tatu hadi Desemba 20,mwaka huu.
Katika kalenda ya kawaida, mkutano huo ulipaswa kufanyika Februari mwakani.
Jana Makinda wakati akiongoza Bunge lililoketi kama kamati kupitia muswada wa marekebisho ya sheria mbalimbali wa 2013, alithibisha baadhi ya marekebisho katika sheria inayogusa mgawanyo wa fedha katika Mfuko wa Elimu (TEA),yatafanywa katika mkutano wa 14 utakaofanyika mwezi ujao.
 “Nadhani tukubaliane na maelezo ya Serikali yaliyotolewa na Mwanasheria Mkuu,tunaweza kuangalia kipengele hicho cha mgawanyo wa hesabu maana tunakutana tena hapa tarehe 3 ya mwezi ujao,”alisema Makinda.
Habari ambazo zimeufikia mtandao wa Fichuo Tz zinasema baada ya Bunge kuahirishwa jana, wabunge watakuwa na wiki moja tu ya mapumziko hadi Novemba 17, watakaposafiri kwenda Dar es Salaam kwa ajili ya kuanza vikao vya kamati Novemba 18.
Mkutano huo wa 14 pamoja na mambo mengine unatarajiwa kujadili Ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), ripoti za mwaka za utendaji za Kamati za Kudumu za Bunge pamoja na kushughulikia miswada ambayo haikuweza kupitishwa katika mikutano ya 12 na 13.
Mabadiliko hayo pia yanalenga kuwezesha Bunge Maalumu la Katiba kufanyika na kuhitimisha kazi yake ifikapo Machi mwaka huu, ili kutoa fursa kwa maandalizi ya Bunge la Bajeti ambalo kwa mujibu wa kalenda hufanyika kati ya Aprili na Julai.
Mpangilio huo wa shughuli mfululizo zinazowahusisha wabunge umeanza kulalamikiwa na baadhi yao kwamba utawaweka mbali na majimbo yao kwa muda mrefu, kuliko ilivyo kawaida.
Waziri wa Nchi,Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi alikiri kuwapo kwa mabadiliko hayo,lakini akasema taarifa rasmi inapaswa kutolewa na Ofisi ya Bunge.
Kabla ya kikao cha Kamati ya Uongozi,Katibu wa Bunge,Dk Thomas Kashililah alikiri kuwapo kwa kusudio la kufanya mabadiliko, lakini akasema zilikuwa zikisubiriwa baraka za kamati hiyo.
Mwanzoni mwa wiki hii,Spika Makinda aliwatangazia wabunge kwamba wanakusudia kufanya mabadiliko kweye kalenda ya Bunge ili kutoa mwanya wa kufanyika kwa Bunge Maalumu la Katiba, bila kuathiri mikutano ya Bunge iliyopo kikatiba

0 comments:

Chapisha Maoni