Jumatatu, Septemba 09, 2013

UKATILI ULIOPITILIZA, MWANAMKE AJIFUNGUA NA KUMTUPA MTOTO CHOONI

Mwanamke mmoja anayedaiwa kuwa ni mke wa mtu, amefanya kitendo cha kinyama baada ya kujifungua msalani na kukiua kichanga chake.

Tukio hilo limetokea hivi karibuni maeneo ya Mazizini, Ukonga Wilaya ya Ilala jijini Dar es Salaam baada ya mwanamke huyo ambaye jina lake halikupatikana kukitumbukiza kichanga hicho chooni. 
 
Kwa mujibu wa chanzo chetu, mwanamke huyo ni mkazi wa Ukonga Moshi Bar amedaiwa kunywa dawa kwa ajili ya kuutoa ujauzito aliokuwa nao wa miezi minane na baada ya kuona hali imebadilika alitoka nyumbani kwake Moshi Bar na kukimbilia Ukonga Mazizini kwa ajili ya kutaka msaada kwa mama yake mdogo.
Baada ya kufika kwa mama yake mdogo aliomba maji kwa ajili ya kwenda chooni, hata hivyo alizunguka nyuma ya choo kwa ajili ya kujipa msaada wa siri lakini hali ilivyokuwa mbaya zaidi, aliamua kuingia ndani ya choo hicho na kujifungua kichanga hicho na kukidumbukiza ndani ya shimo la choo.
Mashuhuda wa tukio hilo wamesema kuwa walimuona mwanamke huyo akibebwa kwenda ndani kwa mama yake mdogo ili aweze kupatiwa msaada zaidi lakini hali ilizidi kuwa mbaya kwa kuanza kuvimba mwili kutokana na kutokwa na damu nyingi.
Waandishi walifanikiwa kuzungumza na mama mdogo wa mwanamke huyo ambaye alijitambulisha kwa jina la mama Athony na kukiri binti huyo kukumbwa na mkasa huo wakati yeye akiwa kwenye shughuli zake.
Mwakilishi wa mjumbe na shina namba 34 Ukonga Mazizini, Bi Mtende amesema kuwa tukio hilo limewashangaza kutokana na mwanamke huyo kwenda kutupa kichanga chooni kwa makusudi.
Kamanda wa polisi Mkoa wa Kipolisi wa Ilala, ACP Marietha Minangi alikiri kutokea kwa tukio hilo ambalo yeye aliliita ni la kikatili na mwanamke huyo amepelekwa katika Hospitali ya Amana kwa matibabu na mwili wa kichanga hicho kimepelekwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa uchunguzi zaidi

0 comments:

Chapisha Maoni