Jumatano, Agosti 28, 2013

KESI YA PONDA...MOROGORO HAKUKALIKI

Kiongozi wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu, Sheikh Ponda Issa Ponda jana alisababisha kusimama kwa shughuli za Serikali wilayani Morogoro baada ya ofisi kadhaa ikiwamo ya Mkuu wa Wilaya na baadhi ya mitaa kufungwa ili kupisha kusikilizwa kwa kesi inayomkabili katika Mahakama ya Mkoa wa Morogoro.

Tofauti na Agosti 19, mwaka huu wakati aliposafirishwa kwa helikopta, jana Sheikh Ponda alisafirishwa kwa barabara kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro akiwa chini ya ulinzi.
Mbali ya Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Morogoro kufungwa, nyingine ni Hazina Ndogo, Madini, Posta, Vipimo, Ukaguzi na Maktaba ya Mkoa.
Sababu za kufungwa kwa ofisi hizo pamoja na Mtaa wa Stesheni na maeneo ya Posta ni kuwa jirani na Mahakama hiyo. Magari yalizuiwa kutembea katika njia na maeneo ya karibu na ofisi pamoja na Mahakama hiyo huku kukiwa na idadi kubwa ya askari polisi na magereza kwa muda wote wa takriban saa mbili.
Alifikishwa mahakamani hapo saa 4:10 asubuhi akiwa katika basi la Magereza ambalo lilisindikizwa na jingine dogo, huku magari mengine yakisimamishwa kupisha msafara huo. Mahakama hiyo ilifurika umati wa wafuasi wa kiongozi kiasi cha kuwalazimu polisi na wana usalama wengine kuweka utepe kuwazuia wengi wao kufika katika jengo lililokuwa likitumika kuendesha kesi hiyo.
Shughuli katika eneo hilo zilirejea katika hali yake ya kawaida saa 6:25 mchana baada kesi yake kuahirishwa na msafara wa Sheikh Ponda kurejea katika Gereza la Segerea, Dar es Salaam ambako yuko rumande.
Muda wote tangu kuwasili mpaka kusikilizwa kwa kesi hiyo, wafuasi hao walikuwa kimya hadi pale ilipoahirishwa na hasa baada ya Sheikh Ponda kuwapungia mkono alipokuwa akielekea kwenye basi ambako walisikika wakisema: “Takbriir na kuitikia Allahu Akbar – (Mungu Mkubwa).”


Kesi yenyewe


Katika kesi hiyo, Wakili wa Serikali, Benard Kongola alisema mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mkoa wa Morogoro, Richard Kabate kuwa Sheikh Ponda alitenda makosa ya uchochezi Agosti 10, mwaka huu saa 11.45 jioni kwenye maeneo ya Kiwanja cha Ndege, Morogoro.
Alisema siku hiyo, Sheikh Ponda alialikwa kutoa maelezo machache kwenye Kongamano la Eid lililoandaliwa na Umoja wa Wahadhiri Mkoa wa Morogoro (Uwamo) na kwamba akiwa hapo alitamka maneno: “Ndugu Waislamu, msikubali uundwaji wa kamati za ulinzi na usalama za misikiti kwani kamati hizo zimeundwa na Baraza la Waislamu Tanzania (Bakwata), ambao ni vibaraka wa CCM na Serikali na kama watajitokeza kwenu watu hao na kujitambulisha kwamba wao ni kamati za ulinzi na usalama za misikiti, fungeni milango na madirisha ya misikiti yenu na muwapige sana,” huku akijua kutoa maneno hayo ni kosa kisheria.
Alisema kwa kufanya hivyo, Sheikh Ponda anayetetewa na mawakili watatu wanaoongozwa na Juma Nassoro, alivunja masharti ya Mahakama ya kifungo cha nje iliyotolewa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ya Mei 9, mwaka huu iliyokuwa imetamka kuhubiri amani.
Katika shtaka la pili, Sheikh Ponda anadaiwa kuwashawishi wafuasi wake kutenda kosa la jinai kwa kuwaambia: Serikali ilipeleka jeshi Mtwara kushughulikia suala la vurugu iliyotokana na gesi kwa kuwaua, kuwabaka na kuwatesa wananchi kwa sababu asilimia 90 ya wakazi wake ni Waislamu, lakini haikufanya hivyo kwa wananchi wa Loliondo waliokataa Mwarabu asipatiwe kipande cha ardhi ya uwindaji baada ya kudai ni mali yao kwa sababu asilimia 90 ya wakazi wake ni Wakristo.” Shtaka la tatu ni kudaiwa kutamka maneno yaliyoumiza imani ya watu wengine kama yalivyo katika shtaka la pili.

0 comments:

Chapisha Maoni