Jumatatu, Machi 28, 2016

RAIS MAGUFULI AWATAKA WATANZANIA KUSHIRIKIANA KUIJENGA NCHI BILA KUBAGUANA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amewasihi watanzania kuendelea kuwa wamoja na kushirikiana kuijenga nchi yao, badala ya kubaguana.
Rais Magufuli ametoa wito huo leo katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Usharika wa Azania Front Jijini Dar es salaam, ambako amesali ibada ya Pasaka pamoja na waumini wa kanisa hilo.
Amesema Mwenyezi Mungu alimtoa mwanae wa pekee Yesu Kristo kuja kuikomboa dunia bila kuwabagua wanadamu, vivyo hivyo nasi binadamu tunapaswa kutobaguana, iwe kwa dini zetu, makabila yetu, mitazamo ya kisiasa na hata rangi zetu.
Aidha, Rais Magufuli amewakumbusha watanzania kufanya kazi kama ambavyo vitabu vitakatifu vinasisitiza umuhimu wa kufanya kazi, na amebainisha kuwa Tanzania yenye neema inawezekana endapo kila mtu atazingatia kufanya kazi.
“Tukifanya kazi hatuhitaji hata misaada kutoka nje, nchi hii ina neema nyingi. Kwa kweli tukifanya kazi kwa bidi nchi yetu inapaswa kuwa inatoa misaada kwa nchi nyingine na sio kuomba misaada kutoka nchi nyingine” Amesisitiza Dkt. Magufuli.
Rais Magufuli ambaye amesali kwenye kanisa hilo kwa mara ya kwanza tangu achaguliwe kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini ikiwa ni mara yake ya nne kusali katika kanisa hilo hata kabla ya kuwa Rais, amewaomba watanzania kuendelea kuliombea Taifa lao na pia kumuombea yeye ili afanikiwe kutekeleza jukumu kubwa na zito la kuiongoza nchi.
Pamoja na kuongoza maombi ya kumuombea Rais Magufuli na Mkewe Mama Janeth Magufuli waliohudhuria ibada hiyo, Askofu Mkuu wa KKKT Dayosisi ya Mashariki na Pwani, Dkt. Alex Malasusa amempongeza Rais Magufuli kwa tabia yake ya kupenda kuhudhuria ibada na kuwasihi viongozi wengine kupenda ibada.
Askofu Malasusa ameuelezea ufufuo wa Yesu Kristo kuwa jambo la kuleta matumaini, na hivyo amepongeza mwelekeo wa nchi kwa sasa, huku akisema Kanisa linaona matumaini kwa Taifa.

0 comments:

Chapisha Maoni