Jumatano, Julai 02, 2014

RPC MBEYA AAGIZA KUKAMATWA MFANYABIASHA MKUBWA

KAMANDA wa Polisi Mkoa wa Mbeya (RPC), Ahmed Msangi, amemwagiza Mkuu wa Polisi (OCD) Wilaya ya Mbarali, Julius Lukindo kumkamata mfanyabiashara Tanu Deminyembe anayedaiwa kupora magunia 450 ya mpunga.
Agizo la kamanda huyo limekuja baada ya uchunguzi wa Tanzania Daima kwa wiki nne kuhusu mfanyabiashara Tanu Deminyembe kuliagiza kundi lake na kwenda kupora mpunga kwa wakulima aliowakopesha fedha kinyume cha mkataba.

Kugundulika kwa mvutano huo kulitokana na mfanyabiashara huyo kuwekeana mikataba na wakulima msimu wa kilimo ili wanapoanza mavuno wamrejeshee magunia ya mpunga na aina ya mbegu anayoihitaji.
Ili kukamilisha biashara hiyo, George Mwanga aliangukia kwenye mikono ya Tanu aliyemkopesha sh milioni mbili na kutakiwa arejeshe magunia 58 ya mpunga aina ya saro baada ya mavuno.
Habari zaidi zinabainisha kwamba mkulima huyo aliporwa magunia mengi ya mpunga kinyume cha mkataba uliopaswa kumalizika jana huku akishuhudia kundi la vijana wakiongozwa na Mwangosi kuingia shambani na kubeba mpunga huo wakidai kuagizwa na bosi wao.
Mwanga alilithibitishia gazeti hili kuwa uporaji ulifanywa shambani kwake na kuchukuliwa magunia yote wakimuacha hana kitu.
Huu ni uporaji, kweli kanikopesha fedha kwa mkataba huu unaouona, hakupaswa kuwatuma watu kuja kuchukua mpunga wangu kabla ya wakati… wamechukua hata mali isiyowahusu, nimekimbilia polisi sijui watanisaidiaje
alisema Mwanga.
Tanu alikiri kumkopesha fedha mkulima huyo na kudai kuwa alichukua magunia 86 ya mpunga kabla ya wakati wa mkataba huku akikana kulituma kundi hilo kwenda kuchukua mpunga.
Huyu mzee alinipigia simu kipindi anataka hela, hao waliokwenda kuchukua mpunga shambani kwake siwafahamu… nilipokuwa Dar aliniomba nimuongezee fedha hata kwa riba mimi nilikataa. Niliporudi nilichukua magunia 86, bado magunia 54 namdai
alisema Tanu.
Kamanda Lukindo alipohojiwa kuhusu uporaji huo, alidai hana taarifa na kumtaka mkulima aliyefanyiwa kitendo hicho afike ofisini ambako alimkutanisha na mfanyabiashara huyo kwa lengo la kuwashauri wamalizane.
Sakata hilo lilifika kwa Kamanda Msangi ambaye baada ya kuhojiwa alimuagiza OCD Lukindo kuwakamata waliohusika na uporaji huo na kuwafungulia kesi ya jinai ili kuliepusha jeshi hilo kuchafuka kwa madai ya kushindwa kufanya kazi.
Habari zilizothibitishwa na Tanzania Daima kutoka Mbarali, ni kwamba mfanyabiashara huyo amekamatwa na msako unaendelea kuwanasa vijana waliochukua magunia 450 ya mpunga.

0 comments:

Chapisha Maoni