Alhamisi, Juni 12, 2014

NUSURA PUNDA AMUUE WAZIRI PROF. ANNA TIBAIJUKA

Waziri wa ardhi nyumba na maendeleo ya makazi Profesa Anna Tibaijuka amenusurika kifo baada ya gari alilokuwa akisafiria kutoka Bukoba kwenda Dodoma kugonga mnyama punda katika kijiji cha Wendele Wilayani Kahama Mkoani Shinyanga.
Walioshuhudia tukio hilo walisema lilitokea jana majira ya saa 11 jioni ambapo gari lenye namba za usajili STK 5857mali ya Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya makazi lililokuwa likiendeshwa na dereva Linusi Eliasi (42) liligonga mnyama punda aliyekatiza ghafla barabarani.
Mkuu wa wilaya ya Kahama mkoani Shinyang'a,Bw Benson Mpesya amethibitisha kutokea ajali hiyo na kuongeza kuwa Waziri Tibaijuka alipata mshtuko baada ya ajali hiyo na ofisi ya mkuu wa wilaya Kahama ilimpatia usafiri mwingine kwa ajili ya kuendelea na safari ili kuhudhuria vikao vya bunge kufuatia gari lake kuharibika.
Hata hivyo mkuu huyo wa wilaya ya Kahama Benson Mpesya amesema waziri Tibaijuka hakuumia katika ajali hiyo na leo ameendelea na vikao vya bunge mkoani Dodoma.
Akielezea zaidi kuhusu ajali hiyo ,Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa wa Shinyanga Kihenya Kihenya amesema Waziri Tibaijuka alikuwa na baadhi ya wanafamilia wake katika gari hilo wakitoka Bukoba kwenda Dodoma kwa ajili ya kuwahi shughuli za Bunge zinazoendelea.
Kamanda Kihenya amesema baada ya kufika katika eneo hilo alikatisha punda katikati ya barabara na katika harakati za dereva kumkwepa ndipo gari hilo lilipomgonga na kisha mnyama huyo kufa papo hapo.
Kihenya alisema kuwa katika ajali hiyo hakuna mtu aliyeumia ila kuna baadhi ya watu waliopata majeraha madogo madogo ikiwa ni pamoja na waziri huyo aliyepata mshtuko kidogo lakini baadaye hali yake iliendelea vizuri.
Hata hivyo katika hali ya mshangao wa watu waliomiminika katika Hospitali ya Wilaya ya Kahama kwa ajili ya kumjulia hali waziri na kumpa pole lakini Waziri huyo na msafara wake walikuwa wakipatiwa matibabu na wauguzi katika Hoteli moja iliyopo pembeni mwa hospitali ya Wilaya Kahama.

0 comments:

Chapisha Maoni