Jumatano, Juni 11, 2014

KIKWETE: TAKWIMU ZITUMIKE IPASAVYO KULETA MAENDELEO

Rais Jakaya Kikwete amezitaka idara na taasisi mbalimbali za serikali pamoja na wadau wa maendeleo nchini kutumia ipasavyo takwimu zilizotolewa na ofisi ya taifa ya takwimu kuleta maendeleo huku akiwataka wataalam wa mipango miji kujipanga kwa kutumia taarifa hizo ili kuondokana na ujenzi holela.
Rais Kikwete ametoa rai hiyo jijini Dar es Saalam, alipokuwa akizindua chapisho la tatu la taarifa za msingi za kidemografia, kijamii na kiuchumi linalotokana na sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012 pamoja na matumizi ya tovuti katika kupata taarifa mbalimbali za sensa ambapo amesema suala la chanjo limechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza vifo vya watoto chini ya miaka mitano huku akielezea mipango ya serikali katika kupunguza vifo vya kina mama wajawazito.
Awali akimkaribisha rais waziri mkuu Mh Mizengo Pinda ametoa rai kwa viongozi wote wakiwemo wanasiasa kuendelea kuhamasisha matumizi ya takwimu za sensa kwa lengo la kuboresha maisha ya wananchi na kuongeza kuwa changamoto zipo katika kutekeleza majukumu yaliyoainishwa katika taarifa hiyo lakini serikali inazifanyia kazi.
Kwa upande wake kamishna wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012 hajati Amina Mrisho Saidi amesema sensa ya mwaka 2012 imekuwa tofauti na miaka mingine kwani tafiti zimeweza kuibua mambo mbalimbali ikiwemo mikanganyiko na migogoro mingi ya kiutawala na kwamba matokeo hayo ya sensa yakitumika vizuri itaweza kutatuliwa bila kuleta athari.
Akisoma taarifa hiyo mbele ya rais mkurugenzi mkuu ofisi ya taifa ya takwimu Bi Albina Chuwa amesema matokeo hayo yamebaini mambo mengi katika jamii ikiwemo asilimia 33 ya kaya zote nchini zinaongozwa na wanawake na tafiti zinaonyesha kuwa ukubwa wa kaya una uhusiano wa moja kwa moja na umaskini huku asilimia nane ya kaya zikiwa hazina vyoo.

0 comments:

Chapisha Maoni