Jumapili, Mei 18, 2014

SABABU ZA WIZI WA WATOTO ZAFAHAMIKA

Kwa muda mrefu kumekuwapo na taarifa za watoto kupotea katika mazingira tofauti, huku baadhi yao wakipatikana na kuunganishwa tena na wazazi wao, lakini wengine hawajaonekana hadi leo.
Wakati wazazi na walezi wa watoto hao wakiwa katika kiza kinene wasijue nini cha kufanya, serikali na wadau wanaoshughulikia masuala ya watoto bado hawajapata jibu la swali; watoto hao wapo wapi? Badala yake wameweka wazi sababu za watoto kupotea au kuibwa.
Uchunguzi uliofanywa katika mikoa mbalimbali nchini kubaini sababu za watoto hao kupotea, umebaini kuwa baadhi ya watoto huondoka nyumbani baada ya kutokea ugomvi kati ya wazazi au walezi wao.
Sababu nyingine ni kuibuka kwa biashara ya watoto wanaouzwa kwa watu ambao hawana watoto, nchini na nje ya nchi na imani za kishirikina zinazochochewa na waganga wa jadi.
Taarifa kutoka polisi zinasema kuwa baadhi ya watoto walioripotiwa kwenye vituo vya polisi kupotea au kuibwa, walibainika kuchukuliwa na mmoja wa wazazi wa mtoto kutokana na migogoro kwenye familia.
Zaidi ya watoto 61 waliripotiwa kuibwa Dar es Salaam katika ya mwaka 2012 na 2013, kati yao wa kiume 28 na wa kike 32.
Taarifa kutoka Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam inaeleza kuwa mwaka 2012 kulikuwa na kesi 29 za wizi wa watoto, ambapo kati yake watoto wanne wa kiume waliibwa hospitalini na watano wa kike walichukuliwa wakiwa nyumbani. Watoto saba pekee kati ya wote walioibwa ndiyo walipatikana.
Mwaka jana kulikuwa na kesi za wizi wa watoto 31, kati yao wa kiume wawili walichukuliwa na watu wasiofahamika wakiwa hospitalini na 17 wakiwa nyumbani. Pia watoto wa kike 12 walipotea mwaka huo. Hadi kufikia Desemba 2013, watoto 21 walikuwa wamepatikana, ambapo kati yao wa kiume 11 na wa kike 10.
Kamanda wa Polisi wa Kinondoni, Camillius Wambura anasema watoto wachanga ndio wanaoibwa huku wenye umri mkubwa kidogo hupotea kutokana na sababu mbalimbali zikiwamo uzembe wa wazazi. Wambura anasema baadhi ya wazazi waliiba watoto wachanga kwa sababu ya kutokuwa na uwezo wa kuzaa, tabia iliyokomaa kutokana na wazazi wa aina hiyo kushindwa kukubali hali waliyonayo.
Akitoa mfano anasema kuwa mama mmoja aliiba mtoto mwenye umri wa wiki mbili Dar es Salaam, lakini alikamatwa siku chache baadaye mkoani Rukwa.
Huyu mama alikuwa akiishi Rukwa, alimrubuni mume wake kuwa ana ujauzito, hivyo kwa kuwa siku za kujifungua zilikuwa zimefika alimwambia mumewe anataka kuja Dar es Salaam kujifungua kumbe alikuwa anakuja kuiba mtoto
anasema.
Mama huyo alipomwiba mtoto alimpa rafiki yake atangulie naye Morogoro ambapo alikwenda kumchukua na kwenda naye Rukwa, hata hivyo mtoto huyo alifariki dunia baadaye. Wambura anazitaja sababu za watoto kupotea kuwa ni pamoja na watoto kutoroka nyumbani baada ya kukithiri kwa migogoro kwenye ndoa na wazazi kutokujali watoto wao.

0 comments:

Chapisha Maoni