Jumapili, Mei 25, 2014

IRANI YASISITIZA KUIMARISHA UHUSIANO NA AFRIKA

Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesisitiza azma ya serikali ya Iran ya kuimarisha mahusiano ya pande zote na nchi za Kiafrika bila ya kizuizi chochote. Dakta Muhammad Javad Zarif aliyasema hayo jana usiku kwenye sherehe za kuadhimisha miaka 51 ya kuasisiwa Umoja wa Nchi Huru za Afrika OAU zilizofanyika mjini Tehran. 

Kwenye sherehe hizo, Dakta Zarif aliongeza kuwa, umoja huo ulikuwa nembo ya uhuru kwa nchi zote za Kiafrika. Kwenye hotuba yake, Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Iran aliwakumbuka na kuwashukuru viongozi wa zamani wa bara la Afrika kutokana na juhudi zao za kuleta usawa na uhuru barani Afrika. Dakta Zarif ameelezea kuwepo ubaguzi na ukoloni mamboleo katika baadhi ya maeneo duniani, na kusisitiza kwamba kuna haja ya kuwepo umoja na mshikamano wa kukabiliana na vitendo hivyo. Kwa upande mwingine, Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Iran amelaani vikali vitendo vya kundi lenye misimamo mikali la Boko Haram nchini Nigeria na kuongeza kuwa, lengo la kundi hilo la kigaidi ni kuchafua taswira ya dini tukufu ya Kiislamu. Naye Muhammad Ahmad Kassule Balozi wa Uganda mjini Tehran ameishukuru Iran kwa kuimarisha mashirikiano na nchi za Kiafrika na kutaka juhudi zaidi zifanyike kwa lengo la kuboreshwa mashirikiano hayo katika sekta binafsi kati ya Iran na bara la Afrika. Sherehe hizo zilihudhuriwa na mabalozi wa nchi kadhaa za kigeni walioko mjini Tehran na shakhsia mbalimbali wa Kiirani na kigeni walioko hapa nchini. Aidha Waziri wa Sheria wa Uganda na Waziri wa  Uchukuzi wa Ivory Coast walikuwa wageni maalumu kwenye sherehe hizo.

0 comments:

Chapisha Maoni