Baada ya matukio ya watu kadhaa kumwagiwa tindikali nchini na
kuacha sintofahamu katika jamii, imebainika kuwa shule ndizo
zinazoongoza kwa kuwa na shehena nyingi ya tindikali ambayo imepatikana
bila kupitia utaratibu unaotakiwa.
Mashambulizi ya kutumia tindikali ambayo
yaliwalenga watu mbalimbali wakiwamo viongozi wa dini, wafanyabiashara
na raia wa kigeni, yameacha hofu miongoni mwa wananchi kutokana na
kutapakaa kwa tindikali mitaani.
Akizungumza na Mwananchi katika mahojiano maalumu,
hivi karibuni jijini Dar es Salaam, Meneja wa Ofisi ya Mkemia Mkuu wa
Serikali, Kanda ya Mashariki, Daniel Ndiyo, alisema imebainika kuwa
watumiaji wa kemikali 748 hawajasajiliwa na ofisi hiyo.
Alisema watumiaji 399 katika hao ni shule za sekondari.
Ndiyo alisema watumiaji hao walibainika katika
operesheni ya kukagua na kusajili watumiaji wa kemikali, iliyofanyika
Septemba na Oktoba mwaka jana.
Kutajwa kwa watumiaji wasiosajiliwa kunaweka
bayana namna ambavyo watu waliokuwa wakitekeleza mashambulizi ya kutumia
tindikali walivyokuwa wakinunua ‘silaha’ hizo kwa urahisi, hasa katika
maduka binafsi na shule za sekondari.
“Eneo kubwa ambalo tulikuwa hatujalikagua ni shule
za sekondari. Shule hizi haziagizi kemikali kutoka nje ya nchi.
Zinanunua kutoka kwa hawa wasambazaji wadogo, kwa hiyo kitu cha kwanza
ambacho tulitaka kufanya ni kuchunguza ili tujue mtu anayeingiza
kemikali nchini anamuuzia nani,” alisema Ndiyo.
Operesheni hiyo ilifanikisha kutambuliwa kwa
wafanyabishara wakubwa 43 wa jijini Dar es Salaam, ambao huingiza
kemikali na kuiuza kwa wateja nchi nzima.
Pia alisema kutokana na kutokuwepo kwa udhibiti
imara wa ununuzi wa kemikali, kuna uwezekano kuwa hata wateja wadogo nao
walikuwa wanauza kwa watu wengine mitaani.
Hata hivyo, Ndiyo hakuwa tayari kutaja aina ya
tindikali ambayo inapatikana kwa wingi mitaani kwa madai kuwa kufanya
hivyo kutachochea watu wasiokuwa na nia njema kuitafuta tindikali hiyo
kwa ajili ya kuwadhuru watu wengine.
Katika kudhibiti madhara makubwa zaidi kutokea,
mtu yeyote haruhusiwi kununua kemikali bila ya kuwa na cheti au kibali
kutoka kwa Mkemia Mkuu kinachomruhusu kununua bidhaa hiyo.
“Hata wafanyabiashara wadogo wa kutengeneza sabuni
wanapaswa waje hapa (Ofisi ya Mkemia Mkuu) wajisalimishe na kujieleza
wao ni kina nani na wanafanya nini, ili waandikiwe barua na kuwekwa
kwenye rekodi kwamba wao wanatumia kufanyia kitu fulani,” alisema.




0 comments:
Chapisha Maoni