Jumanne, Oktoba 22, 2013

KANSA YA MATITI BADO HATARI KUBWA TANZANIA

Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dk Marina Njelekela amesema saratani ya matiti inaongoza kwa kuwa na waathirika wengi zaidi ukilinganisha na saratani nyingine.
Akifungua mafunzo ya kuwapiga msasa madaktari wa upasuaji wa matiti, Dk Njelekela alieleza kuwa kwa kipindi cha mwaka mmoja jumla ya wagonjwa 856 waliofanyiwa upasuaji katika vitengo viwili vya upasuaji kati yao 162 waligundulika kuwa na saratani ya matiti.
“Yapo magonjwa mengi yanayoshambulia matiti yakiwamo vivimbe na maambukizi, lakini saratani inaonekana kuzidi kuwa tishio kwa wanawake ndiyo maana tumeamua kuendesha mafunzo haya ili kuwapa ujuzi zaidi madaktari” alisema Dk Njelekela.
Alisema kutokana na hali hiyo, Hospitali ya Taifa ya Muhimbili imeamua kutoa mafunzo kwa madaktari wa hospitali kadhaa za Jiji la Dar es salaam zikiwamo za Temeke, Amana, Mwanayamala, Regency na IMTU ili kujifunza tiba na njia mpya za kukabiliana na tatizo hilo.
Kwa upande wake, mwezeshaji wa mafunzo hayo ambaye ni Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Wanawake kutoka Ugiriki, Profesa Zervoudis Stephane alikiri kuwepo ongezeko kubwa la wagonjwa wa saratani ya matiti duniani na matibabu yake pia yamekuwa yakibadilika kila siku kulingana na ukuaji wa teknolojia.
Kwa mujibu wa Profesa Stephane, upasuaji unafanyika kwa teknolojia ya hali ya juu zaidi ambapo sindano huchomwa katika eneo husika na kufuatiwa na upasuaji mdogo ili kuondoa sehemu iliyoathirika.

0 comments:

Chapisha Maoni