Jumanne, Mei 16, 2017

ZUMA BADO HATAKIWI SOUTH AFRICA

Kwa mara nyingine tena mvutano wa kisiasa umeigubika nchi ya Afrika Kusini kiasi kwamba, maelfu ya wapinzani wa serikali wameendelea kufanya maandamano katika siku za hivi karibuni wakitaka Rais Jacob Zuma wa nchi hiyo ajiuzulu.
Maelfu ya wapinzani wamefanya mkusanyiko mkubwa jirani na jengo la Mahakama ya Katiba mjini Johannesburg na kutangaza kwamba, mudhahara na mkusanyiko huo wa malalamiko utaendelea hadi pale Rais Zuma atakapojiuzulu na kuachia madaraka ya nchi. Baleka Mbete, Spika wa Bunge la Afrika Kusini amesema kuwa, wapinzani hao wamewasilisha barua ya mashtaka dhidi ya serikali kuhusiana na kura ya siri ya kutokuwa na imani na serikali katika Bunge la nchi hiyo. Mahakama hiyo inatarajiwa kutangaza msimamo wake kuhusiana na upigaji kura wa siri kuhusiana na kutokuwa na imani na Rais Jacob Zuma.
Licha ya kuwa kabla ya hapo pia Rais Zuma aliandamwa na wimbi la upinzani kutokana na tuhuma za ufisadi wa fedha na wapinzani kumtaka ajiuzulu, lakini duru mpya ya mivutano baina ya serikali yake na wapinzani ilianza mwishoni mwa mwezi Machi, baada ya Rais huyo kulifanyia marekebisho baraza lake na mawaziri na kumtupa nje ya baraza hilo Pravin Gordhan aliyekuwa Waziri wa Fedha.
Akihalalisha uamuzi wake huo, Rais Zuma alisema kuwa, mabadiliko hayo yalifanyika katika fremu ya juhudi za kuboresha hali ya uchumi na kuondoa vizingiti vya sasa vya kiuchumi. Hata hivyo watu wengi wanaamini kwamba, mabadiliko hayo yalitokana na vita vya madaraka ndani ya chama tawala cha ANC na kwamba, kufutwa kazi Pravin Gordhan kulifanyika kwa matashi ya kisiasa.
Pravin Gordhan alikuwa waziri kuanzia mwaka 2009 hadi 2014 na baadaye mwishoni mwa mwaka jana akateuliwa tena kushika wadhifa huo. Tangu alipoteuliwa tena kuchukua wadhifa wa Waziri wa Fedha, Pravin Gordhan amekuwa na mivutano na shakhsia wa kisiasa wa chama tawala cha ANC. Mivutano baina ya Pravin Gordhan na wanasiasa hao ilianza baada ya waziri huyo aliyefutwa kazi kusisitiza juu ya ulazima wa kupambana na uongozi mbaya na kuweko marekebisho katika muundo wa mashirika ya kiserikali nchini.  Aidha alisisitiza mara chungu nzima juu ya ulazima wa kupambana na ufisadi. 
Pravin Gordhan alikuwa na mpango wa kupunguza matumizi ya serikali, aongeze kodi na kuifikisha nakisi ya bajeti ya nchi hadi asilimia 3.2 ya uzalishaji malighafi katika mwaka wa fedha wa 2016-2017. Mbali na kuibuka mivutano iliyotokana na kuuzuliwa waziri huyo, kuenea ufisadi, kukosekana nafasi za ajira na kupungua kiwango cha ukuaji uchumi ni sababu nyingine zinazotajwa na wajuzi wa mambo kwamba, zimepelekea kuongezeka malalamiko katika nchi hiyo dhidi ya serikali.
Afrika Kusini ni moja ya nchi zinazosafirisha nje ya nchi madini, lakini kwa miaka kadhaa ya hivi karibuni kutokana na kupungua bei ya madini chimbuko lake likiwa ni kupungua wateja hususan wanunuzi wakubwa kabisa kama China, imekuwa ikikabiliwa na matatizo ya kifedha na kiuchumi. 
Kuongezeka kiwango cha kupanda gharama za maisha, kukata tamaa wawekezaji, mashirika na watumiaji kuhusu mustakabali wa uchumi wa Afrika Kusini ni sababu nyingine ya kudorora kiwango cha ukuaji uchumi wa nchi hiyo.  Hii ni katika hali ambayo, katika miaka kadhaa ya huko nyuma, Afrika Kusini ilikuwa nchi yenye mafanikio makubwa zaidi ya ukuaji wa uchumi.
Suala la kupambana na ufisadi lingali ni takwa la akthari ya wapinzani wa Rais Jacob Zuma. Wapinzani wanamtuhumu Zuma kwamba, hapambani na ufisadi na rushwa kama inavyotakiwa.
Hivi sasa sio wapinzani tu wanaotaka Rais Zuma ajiuzulu, bali hata maveterani wa vita vya ubaguzi wa rangi nchini humo, wanaharakati wa chama tawala, muungano wa wafanyakazi na makundi ya kiraia nchini humo nayo yamejiunga katika safu ya wanaotaka Zuma aachie ngazi kabla ya kumalizika muhula wake wa pili wa uongozi.
Akthari yao wana wasiwasi kwamba, kupungua uungaji mkono wa wananchi kwa chama hicho kutakuwa na taathira hasi kwa chama hicho katika uchaguzi mkuu ujao wa 2019. Pamoja na hayo yote, Rais Zuma amesisitiza kuwa, atabakia madarakani hadi muhula wake wa kisheria utakapomalizika.

0 comments:

Chapisha Maoni