Wajumbe wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) kupitia kwa
Mwenyekiti wao Freeman Mbowe, wamemjibu Rais Kikwete wakisema watakuwa
radhi kurudi Bunge la Katiba endapo kutafanyika taathmini na tafakuri ya
kina katika kubaini sababu za kuvurugika kwa Bunge hilo na kuzitazama
kanuni zinazolisimamia, pamoja na sheria ya mabadiliko ya katiba.
Pia UKAWA wametaka pawepo na makubaliano ya maandishi kwamba hakutakuwa na kauli za matusi, kudharauliana wala kejeli, bali kitakachojadiliwa ni maoni ya wananchi yaliyomo kwenye rasmu ya Tume ya Jaji Warioba.
Msimamo huo ulitolewa juzi na Mhe.Mbowe ambaye pia ni Mwenyekiti wa
CHADEMA Taifa, alipokuwa akizungumzia mchakato huo wa Katiba mpya
Wilayani Hai mkoani Kilimanjaro, baada ya UKAWA kuwa wameombwa na
Viongozi mbalimbali warudi Bungeni.
Alisema kuwa Viongozi
mbalimbali akiwemo Rais Kikwete na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda,
wamewaomba warudi kwenye Bunge hilo, lakini wai wametoa masharti kwamba
kufanyike vikao vya pamoja vya kutathmini hali iliyojitokeza awali,
kisha wawekeane utaratibu wa kufuata kimaandishi.
Uwendawazimu ni kufanya mambo yale yale kwa kutumia watu wale wale na kwa utaratibu ule ule, halafu utegemee matokeo tofauti. Tumetoka kwenye Bunge la Katiba ambapo tumeona matusi, kejeli, dharau, ubaguzi wa hali ya juu na kupuuzwa kwa maoni ya wananchi, halafu mnatuita turudi kwenye Bunge lile lile tukatukanane kisha mtegemee kupata Katiba bora
Alihoji Mbowe.
Mbowe ambaye pia ni Kiongozi wa Kambi rasmi ya upinzani Bungeni,
alisisitiza kuwa, hata wakikubaliana wakarudi kisha matendo yale ya
awali yakajitokeza ikiwemo kupuuza maoni ya wananchi, hawatasita kutoka
tena kwa lengo la kupigania kupatikana kwa Katiba bora yenye kuzingatia
maslahi ya wananchi wote.
Mhe.Mbowe alisema kuwa, Wabunge wa CCM
hawawezi kuhitimisha mchakato huu wakiwa peke yao, kwa kile alichoeleza
kuwa, Katiba inatakiwa kuandaliwa na makundi yote ya jamii.
0 comments:
Chapisha Maoni