Jumatatu, Januari 20, 2014

SASA MAKUBALIANO GENEVA KUANZA UTEKELEZAJI

Hatimaye baada ya kusubiriwa kwa muda, hatua ya kwanza ya makubaliano ya nyuklia ya Geneva kati ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na kundi la 5+1 imeanza kutekelezwa leo.
Kwa mujibu wa hatua ya kwanza ya utekelezaji wa makubaliano ya Geneva yaliyotiwa saini tarehe 24 Novemba kati ya Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Iran na kundi la 5+1, pande hizo mbili zimeaanza leo kutekeleza ahadi zao ikiwa ni pamoja na kusimamisha vikwazo dhidi ya Iran na Tehran kusimamisha urutubishaji wa madini ya urani kwa asilimia 20.
Wasimamizi wa Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Atomiki pia waliwasili nchini Iran Ijumaa iliyopita kwa ajili ya kusimamia utekelezaji wa hatua kwa hatua wa makubaliano hayo. Kwa msingi huo Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na kwa hiari yake itahifadhi nusu ya urani iliyorutubishwa kwa asilimia 20 kwa ajili ya kuzalisha nishati ya tanurinyuklia ya utafiti ya Tehran na nusu inayobakia itabadilishwa na kuwa urani iliyorutubishwa kwa asilimia 5. Iran pia itatangaza kuwa katika kipindi cha miezi sita ijayo ya awamu ya kwanza ya utekelezaji wa makubaliano ya Geneva haitarutubisha unanium kwa zaidi ya asilimia 5.

Mkuu wa Shirika la Atomiki la Iran Ali Akbar Salehi amesema kuwa hatua muhimu zaidi ya kwanza inayochukuliwa na Iran ni kusimamisha kwa hiari urutubishaji wa madini ya urani kwa asilimia 20 ambao unaanza leo katika vituo vya Natanz na Fordow. Salehi amesema urutubishaji wa madini ya urani kwa asilimia 20 haukuwa kabisa katika ajenda za nyuklia za Iran lakini wataalamu wa nyuklia hapa nchini walichukua uamuzi wa kurutubisha urani kwa kiwango hicho baada ya kumalizika nishati ya kituo cha utafiti cha Tehran na wakati Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Atomiki (IAEA) ulipokataa kutekeleza majukumu yake ya kudhamini nishati hiyo.
Sambamba na hatua hizo zinazochukuliwa na Iran, Umoja wa Ulaya pia hii leo umeanza kupunguza na kuondoa vikwazo vyake dhidi ya Iran. Kwa mujibu wa hatua ya kwanza ya utekelezaji wa mkataba wa Geneva vikwazo vyote vya petrokemikali dhidi ya Iran vitaondolewa. Vilevile nchi hizo zitaiondolea Iran vikwazo vya dhahabu, madini mengine yenye  thamani na usafirishaji.
Kwa utaratibu huo mwenendo wa kutatua hitilafu juu ya faili la nyuklia la Iran ambalo lilianzishwa bila ya sababu yoyote umeanza leo kwa kuanza kutekelezwa awamu ya kwanza ya makubaliano ya Geneva. Hatua hii kwa hakika itathibitisha nia njema ya pande mbili ya kutekeleza ahadi zao.

0 comments:

Chapisha Maoni