Jumatatu, Desemba 09, 2013

DIDIER DROGBA NA EMMANUEL EBOUE WAADHIBIWA KWA KUMUENZI

Shirikisho la Soka la Uturuki limewatia hatiani wachezaji wawili wa kimataifa kutoka Ivory Coast Didier Drogba na Emmanuel Eboue wanaosakata kabumbu kwenye klabu ya Galatasaray ya nchini Ururuki kwa kosa la kuonyesha heshima na kumuenzi  hayati Nelson Mandela, baada ya kumalizika mechi ya ligi ya nchi hiyo.
Magazeti ya Milliyet na Hurriyet yanayochapishwa Uturuki yameandika kuwa, Drogba anakabiliwa na kosa hilo baada ya kumalizika mechi kati ya klabu yake ilipopambana na SB Elazigspor siku ya Ijumaa. Drogba  alivua jezi na kubakisha fulana ya ndani iliyosomeka maandishi "Thank You Madiba". Taarifa zinasema kuwa, Eboue naye anakabiliwa na kosa kama hilo ambapo yeye  fulana yake ya  ndani iliandikwa 'Rest in Peace Nelson Mandela'. 
Nelson Mandela alikuwa kiongozi aliyepambana na utawala wa ubaguzi wa rangi nchini Afrika Kusini, na alifariki dunia  Alhamisi iliyopita akiwa na umri wa miaka 95. Shirikisho la Soka la Uturuki limetangaza kuwa, wachezaji hao wawili watakabiliwa na adhabu ya utovu wa nidhamu kwa kuvunja sheria ya shirikisho hilo inayokataza wachezaji kuvaa fulana zinazotoa jumbe na nara za kisiasa.

0 comments:

Chapisha Maoni