Alhamisi, Oktoba 31, 2013

KESI YA KENYATTA ICC IMEPOA

Inawezekana kuwa kesi dhidi ya Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta  katika Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC ikaanza mwaka ujao badala ya mwezi ujao wa Novemba kama ilivyokuwa imepengwa awali.
Shirika la habari la Reuters limeripoti kuwa waendesha mashtaka wa ICC wamesema hawapingi pendekezo la kuakhirisha kesi hiyo.
Viongozi wa Umoja wa Afrika wamekuwa wakishinikiza kesi hiyo isikilizwe nchini Kenya na wengine wakitaka iakhirishwe kwa muda wa mwaka mmoja. Aidha baadhi ya viongozi wa Afrika wametoa wito kwa rais wa Kenya asifike mbele ya ICC kwa msingi kuwa mahakama hiyo inawalenga tu Waafrika na kupuuza mamlaka ya kujitawala Kenya.
Rais Kenyatta na Naibu wake William Ruto wanakabiliwa na tuhuma za kuchochea ghasia za baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2007 ambapo watu 1,200 walipoteza maisha.
Kesi dhidi ya Kenyatta imepata pigo mara kadhaa baada ya mashahidi wa upande wa mashtaka kujiondoa.

0 comments:

Chapisha Maoni