Jumamosi, Oktoba 05, 2013

HIKI NDICHO ALICHOKIONGELEA RAIS KIKWETE KATIKA HOTUBA YAKE JUU YA SHAMBULIZI LA WESTGATE NA USALAMA TANZANIA

Ndugu Wananchi;    
Wakati nikiwa safarini, tarehe 21 Septemba, 2013  kulitokea shambulilizi la kigaidi katika Jengo la Biashara la Westgate, huko Nairobi, Kenya.  Watu 67 walipoteza maisha na zaidi ya 200 walijeruhiwa.  Nilituma salamu za pole na rambirambi kwa Mheshimiwa Rais Uhuru Kenyatta na wananchi wa Kenya na kuwahakikishia kuwa tupo pamoja nao katika wakati huu wa majonzi.
Nafahamu kuwa baada ya tukio hilo watu wengi hapa nchini wameingiwa na hofu kuhusu usalama wetu.  Ni hofu ya msingi kwani tarehe 8 Agosti, 1998 Ubalozi wa Marekani hapa nchini ulishambuliwa na magaidi na ndugu zetu 11 wasio na hatia walipoteza maisha. 
Ndugu Wananchi;
Napenda kuwafahamisha kuwa tangu shambulio la mwaka 1998, Serikali imekuwa inajenga uwezo wa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama kupambana na ugaidi katika nyanja mbalimbali.  Tunaendelea kujiimarisha bila kusita siku hadi siku.  JWTZ, Polisi na Idara ya Usalama wa Taifa wamekuwa na ushirikiano wa karibu kwa ajili hiyo.  Juhudi zetu hizo ndizo zinazotufanya tuwe salama hadi sasa.

Baada ya tukio la Kenya, vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vimeimarisha mikakati yao maradufu.  Pamoja na kujizatiti kwetu huko hatuwezi kusema kuwa tukio la kigaidi halitaweza kutokea nchini.  Uhakika huo hatuna kwani hata mataifa makubwa na tajiri yameshambuliwa.  Kilicho muhimu ni kuendelea kuchukua tahadhari na wananchi kusaidia ili  vyombo vyetu vifanikiwe zaidi.    
Hali kadhalika, tumewataka watu wote wenye shughuli zinazokusanya watu wengi kama vile maduka, maofisi, mahoteli, migahawa n.k. waweke kamera za ulinzi nje na ndani ya maeneo yao.  Pia waangalie uwezekano wa kuweka vifaa vya upekuzi (metal detectors and x-rays).  Najua watu wanaweza kulalamikia usumbufu au gharama, lakini gharama na hasara ya kushambuliwa ni kubwa zaidi kuliko ya usumbufu huo.
Ndugu Wananchi;
Nawaomba muendelee kufanya shughuli zenu bila ya hofu ingawaje msiache kuwa makini na kuchukua tahadhari.  Watu watoe taarifa kwa vyombo vya usalama wanapoona mtu au watu au kitu cha kutilia shaka.  Ni muhimu kwa usalama wake, wa kila mtu, jamii na taifa.  Maafisa husika wa vyombo vya ulinzi na usalama wataendelea kuelimisha umma kuhusu hatua mbalimbali za tahadhari za kuchukua.  Sisi Serikalini tumejipanga kuchukua hatua zaidi kuimarisha ulinzi na usalama wa nchi yetu na watu wake.

0 comments:

Chapisha Maoni