Jumatano, Julai 02, 2014

KAULI YA MAASKOFU KWA UKAWA

Baraza la Maaskofu la Kanisa Katoliki Tanzania (TEC), limewataka wajumbe wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), kurudi bungeni bila masharti na kuendelea na mjadala wa Katiba kwa manufaa ya taifa.
Pia, Askofu wa Kanisa la Tanzania Assemblies of God (TAG), Jimbo la Mashariki Kaskazini, Geoffrey Massawe amewaomba wajumbe wa Bunge la Katiba kuungana na kuwa kitu kimoja katika mchakato wa kujadili Rasimu ya Mabadiliko ya Katiba.
Kauli hizo za maaskofu hao zimekuja siku moja baada ya ile ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kusema kuwa hatima ya uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwaka huu utategemea Ukawa, kurejea katika Bunge Maalumu kuipitisha Katiba Mpya kwa wakati.
Askofu Massawe alitoa ombi hilo wakati wa ibada maalumu ya sherehe ya maadhimisho ya miaka 75 tangu kuanzishwa kwa kanisa hilo nchini iliyofanyika katika Kanisa la TAG Kinondoni, Dar es Salaam.
Akitoa salamu za TEC wakati wa kuadhimisha miaka 25 ya uaskofu ya Mhashamu Tarcisius Ngalalekumtwa kwenye Uwanja wa Kichangani, Iringa, Makamu Rais wa TEC, Mhashamu Severine Niwemugizi alisema ni vyema wajumbe hao wakarudi kwenye Bunge hilo linalotarajia kuanza Agosti 5, mwaka huu.

0 comments:

Chapisha Maoni