Jumamosi, Julai 05, 2014

CHANZO CHA NGASA KUTEMWA TAIFA STARS

WAKATI msafara wa timu ya soka ya Tanzania, Taifa Stars ukitarajiwa kurejea nchini kesho ukitokea kambini nchini Botswana, kuna habari kuwa Kocha Mart Nooij, amemtema mshambuliaji Mrisho Ngasa kwa utovu wa nidhamu.
Hiyo ni baada ya nyota huyo kushindwa kusafiri na wenzake nchini Botswana na kwenda nchini Afrika Kusini kufanya majaribio ya kucheza soka ya kulipwa na kufuzu, hivyo kusubiri baraka za klabu yake ya Yanga.
Chanzo cha uhakika kilichopo karibu na Nooij, kimedokeza kutoka Botswana kwamba kocha huyo amemtema Ngasa kutokana na kukerwa na kitendo chake cha  kushindwa kutambua nafasi yake kwa Stars kuelekea mechi ya Julai 20 dhidi ya Msumbiji.
Chanzo hicho kimedokeza kuwa kitendo cha nyota huyo kushindwa kuungana na wenzake, hivyo kukosa mazoezi muhimu kuelekea mechi hiyo dhidi ya Msumbiji, kocha haoni sababu ya kuendelea kumng’ang’ania kwani suala la timu ya taifa linahitaji utashi binafsi.
Stars itawakaribisha Msumbiji katika mechi ya kwanza kati ya mbili za kuamua timu ya kuingia katika kundi F, kuungana na Zambia, Niger na Cape Verde katika mbio za kuwania tiketi ya fainali za Mataifa Afrika mwakani nchini Morocco.
Katika hatua nyingine, Stars inatarajia kurejea nchini saa 12:15 jioni na kuendelea kujifua kwa mechi hiyo itakayochezwa Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.

0 comments:

Chapisha Maoni