Jumapili, Mei 18, 2014

USHINDI WA TAIFA STARS JANA DHIDI YA ZIMBABWE

Mashabiki wa soka wa Tanzania, jioni leo wameondoka uwanjani kifua mbele baada ya kuishuhudia timu yao ya Taifa, Taifa Stars, ikiibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Zimbawe, mechi iliyopigwa katika Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.
Mechi ya Stars na Zimbabwe ni ya kuwania kufuzu kucheza Kombe la Mataifa ya Afrika yatakayofanyika mwaka 2015, ambapo Stars imejiweka katika nafasi nzuri kabla ya mechi ya marudiano itakayopigwa wiki mbili zijazo nchini Zimbabwe.
Bao la Stars lilifungwa dakika ya 13 na John Bocco, huku akilifunga kwa shuti kali nje ya 18, akitumia vyema pasi ya Thomas Ulimwengu.

Awali mpira ulianza kwa kasi, kila timu ikisaka bao la mapema katika mechi hiyo iliyokuwa na ushindani mkubwa kutoka kwa timu hizo.
Nyota wa Stars wakiongozwa na Mbwana Samatta, Ulimwengu, Bocco na Mrisho Ngassa na wengine walifanya juhudi kuibuka na ushindi katika mechi hiyo iliyokuwa na msisimko wa aina yake.
Dakika ya 13 Bocco anaipatia Stars bao la kwanza akipiga shuti kali nje ya 18, akitumia vyema krosi ndefu ya Ulimwengu.
Hata hivyo, mpira ulikuwa ukichezwa kwa rafu za kuvizia, huku mwamuzi Joseph Odartel wa Ghana, kuwa mkali kwa wachezaji wote, akiwamo Milton Mkude aliyeonyeshwa kadi ya njano kwa kumfanyia madhambi Samatta.
Hadi kipindi cha kwanza kinamalizika, Stars walitoka kifua mbele kwa kupata bao hilo moja lililofungwa na Bocco.
Dakika ya 46, Bocco alikosa bao la wazi kutokana na kufanya papara wakati anauwahi mpira na kujikuta akianguka chini. Bocco alishindwa kuitumia krosi ya Ulimwengu.
Wakati Stars wanaendelea kusaka bao jingine, walijikuta Ulimwengu naye akionyeshwa kadi ya njano na mwamuzi aliyeonyesha umakini na ukali kwa wachezaji waliokuwa wakicheza rafu.
Kipindi cha pili Zimbabwe walirudi kwa kasi wakitaka kusawazisha, lakini walishindwa kutokana na uimara wa wachezaji wa Taifa Stars.
Zimbabwe walifanya mabadiliko kwa kumtoa Peter Moyo na kuingia Kudakwashe Musharu, lakini mabadiliko hayo hayajazaa matunda kwao, zaidi ya kushuhudia mchezaji wao Stephen Alimenda akionyeshwa kadi ya njano baada ya kumchezea madhambi Mwinyi Kazinmoto.
Kocha wa Stars, Mart Noij alimtoa Fank Domayo na kuingia Amri Kiemba, wakati Mrisho Ngassa alitoka na nafasi yake kuchukuliwa na Haruna Chanongo, huku Bocco akitoka na nafasi yake kuingia Khamis Mcha.
Hadi mwisho wa mchezo huo Stars walifanikiwa kutoka uwanjani kwa ushindi wa bao 1-0, huku ushindi huo ukiiweka pazuri timu hiyo kwa mechi ya marudiano itakayochezwa wiki mbili zijazo nchini Zimbabwe.
Stars: Deogratius Munish, Shomari Kapombe, Oscar Joshua, Nadir Haroub Cannavaro, Kelvin Yondan, Frank Domayo, Mrisho Ngassa, Mwinyi Kazimoto, Jonh Bocco, Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu.
Zimbabwe: George Chigova, Partson Jaure, Danny Phiri, Hardlife Zvirekwi, Stephen Alimenda, Tendai Ndoro, Milton Mkude, Kudakwashe Mahachi, Cuthbert Malajila, Peter Moyo na Eric Chipeta.

0 comments:

Chapisha Maoni