Jumatatu, Machi 03, 2014

WATANZANIA 13 WASHIKILIWA KWA WIZI MADAGASCAR

Watanzania 13 wametiwa mbaroni nchini Madagascar wakituhumiwa kukutwa na meli iliyosheheni magogo ya miti adimu na ghali ambayo yamepigwa marufuku kuvunwa humo.
Shirika la Habari la Ufaransa (AFP), limesema Watanzania hao wanashikiliwa tangu wiki iliyopita. AFP lilieleza kuwa meli hiyo ambayo inadaiwa kusajiliwa Tanzania, ilikutwa ikiwa imesheheni magogo hayo katika ufukwe wa Madagascar baada ya kupata hitilafu.
Mkurugenzi wa Upelelezi na Usalama wa Jeshi la Polisi Madagascar, Anthony Rakotoarison alikaririwa akisema meli hiyo ilikutwa imebeba magogo 2,135 aina ya rosewood.
Kwa mujibu wa Kamusi ya Tuki, Toleo la Tatu, rosewood ni mwaridi ikisema ni mti mwekundu na mgumu unaotumika kutengeneza samani.
“Ilikuwa ni meli ya Tanzania ambayo ilikuwa imepata hitilafu, tumeikamata,” alisema Rakotoarison.
Pakotoarison alisema walichunguza na kubaini magogo hayo ya miti migumu yenye rangi nyekundu ambayo alisema hayapatikani kwa wingi nchini humo hivyo kuilazimu serikali kupiga marufuku uvunaji wake ili miti hiyo isiteketee.
Alisema miti hiyo ilipata heshima kubwa kimataifa na mahitaji yake yameongezeka kuanzia mwaka 2009.
Hivi karibuni, Rais wa Madagascar, Rais Hery Rajaonarimampianina alipiga marufuku biashara ya miti hiyo.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Uhusiano wa Kimataifa, Michael Haule alisema kuwa bado Serikali ya Tanzania haijapata taarifa kuhusu kukamatwa kwa Watanzania hao pamoja na meli yao.
“Bado sijapata taarifa hizo… Nitafuatilia na nitakujibu,” alisema Haule.
Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini, Advera Senso alisema ofisi yake inawasiliana na Polisi wa Kimataifa nchini (Interpol) ili kupata undani wa habari hizo.

0 comments:

Chapisha Maoni