Jumapili, Februari 09, 2014

SERIKALI YA TZ HUPOTEZA SH. TRILIONI 1.6 KILA MWAKA, SABABU IKO HAPA

Serikali inapoteza Shilingi trilioni 1.6 kila mwaka kutokana na kuzalisha umeme wa mafuta mazito. Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini, Victor Mwambalasa, aliyasema hayo jana jijini Dar es Salaam, wakati  kamati ilipotembelea bandarini ya Dar es Salaam.
Wajumbe wa kamati hiyo walishuhudia  shehena ya mwisho ya mabomba 269 ya mradi wa bomba la  gesi yaliyoagizwa kutoka China ikisafirishwa kwenda Mtwara.
 
Alisema  miundombinu ya bomba hilo  ikikamilika itaokoa  Sh trilioni 1.6 zinazopotea kila mwaka kutokana na mitambo inayotumia mafuta mazito kufua umeme.
 
Aliongeza kuwa, hivi sasa zaidi ya nusu ya umeme unaozalishwa nchini unatokana na gesi asilia na kwamba kwa muda mrefu serikali iliazimia kutumia nishati hiyo kufidia pengo la mahitaji ya umeme kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa na ukame, unaokwamisha umeme wa maji.
 
Mabomba hayo yalikuwa yakipakuliwa kutoka katika meli ya China yenye urefu wa mita 180 na kuingizwa kwenye malori yanayoyapeleka Mtwara.
Mwambalasa amewaomba wadau kuwa wajumbe wa kuelimisha wananchi wenye  lengo la kupotosha ukweli kuhusu mradi huo.
 
“Ikumbukwe kuwa  lengo la serikali ni kuboresha maisha ya wananchi  kwa kupunguza umaskini,” alisema.
 
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliachim Maswi,  alisema mradi huo utakapokamilika, tatizo la umeme  litamalizika na kubakia  historia.
 
"Ndiyo maana leo kamati yenu imekuja bandarini kushuhudia hili, lakini pia zipo ziara mbalimbali zinazofanywa kule Mtwara na mwezi ujao Makamu wa Rais, Dk. Mohammed Gharib Bilal atakwenda," alisema.
 
Alisema kilometa 499 za mkuza wa bomba (njia)  zimekamilika ikiwa ni asilimia 99 ya kazi hiyo.
 
Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli (TDPC), Yona Killagane,  akielezea kuhusu ujenzi wa bomba hilo alisema  umekamilika kwa asilimia 45.
 
Alisema usimikaji wa mitambo unatarajiwa kukamilika mwanzoni mwa mwezi Desemba na majaribio ya mitambo yatafanyika mwezi huo.
 Alisema tayari zaidi ya kilometa 280 za  mabomba yameshapangwa kwenye mkuza.
 
Kuhusu uwekaji wa mabomba kwenye njia yake na kuweka mkongo wa mawasiliano sambamba na bomba alisema kilometa zaidi ya 90 zimekamilika.
 
Alisema ujenzi wa bomba hilo unaotarajiwa kukamilika Mei mwakani ulianza  mwezi uliopita na kwamba hadi sasa zaidi ya kilometa nne zimekamilishwa.

0 comments:

Chapisha Maoni