Jumatano, Februari 19, 2014

KIM POULSEN KULIPWA SH. 420 KAMA FIDIA ENDAPO ATAFUKUZWA KAZI TAIFA STARS

Kocha wa timu ya Taifa (Taifa Stars), Kim Poulsen atalikamua Shirikisho la Soka nchini (TFF), Sh. milioni 420 endapo likifikia uamuzi wa kuachana naye kabla ya mkataba wake kumalizika Mei mwakani.
Rais wa shirikisho hilo, Jamal Malinzi alisema jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki kuwa hatma ya kocha huyo itajulikana Februari 24, mwaka huu (Jumatatu ijayo).
“Kwa sasa siwezi kueleza chochote kuhusu Poulsen kwa sababu si wakati mwafaka wa kuzungumzia suala hilo. Februari 24, mwaka huu kila kitu kitafahamika, tuombe uzima tu,” alisema Malinzi huku taarifa kutoka ndani ya shirikisho hilo zikidai kuwa wamejipanga kumtupia virago raia huyo wa Denmark ikiwa ni sehemu ya mikakati ya kuboresha kikosi cha Taifa Stars.
Alipotafutwa na NIPASHE jijini mwishoni mwa wiki, Poulsen alisema hajali kinachozungumzwa kuhusu kuvunjwa ama kutovunjwa kwa mkataba wake.
“Ninachojali ni kazi yangu, natekeleza majukumu yangu kama kocha wa timu ya taifa bila kujali yanayozungumzwa,” alisema Poulsen.
Kwa mujibu wa Ripoti ya Kamati Maalum ya Kudhibiti na Kuboresha Mapato ya TFF iliyotolewa Mei 2011, kocha wa Taifa Stars analipwa mshahara wa Sh. milioni 315 kwa mwaka (Sh. milioni 26.25 kwa mwezi), kama TFF ikisitisha mkataba wa Poulsen, italazimika kumlipa Sh. milioni 420 ambazo ni mshahara wake wa miezi 16 iliyobaki kuanzia mwezi huu kabla ya kumalizika kwa mkataba wake Mei mwakani.
Ukurasa wa tano wa kiambatanisho cha 7(A) cha ripoti hiyo yenye jumla ya kurasa 95 na viambatanisho tisa unafafanua kuwa jumla za gharama za kocha wa Taifa Stars kwa mwaka ni Sh. milioni 416 ikiwa ni mshahara, nyumba (Sh. milioni 45), usafiri wa kwenda kwao na kurudi (Sh. milioni 20.4), usafiri wa ndani (Sh. milioni 33.6) na bima ya afya (Sh. milioni mbili.
Pengine gharama hizi kubwa ndizo zinazousukuma uongozi mpya wa TFF, ambao umeshaeleza kuvutiwa na makocha wazawa, kufikiria kumtema kocha huyo wa zamani wa timu ya taifa ya vijana wenye umri chini ya miaka 18 (U-18) ya Singapore.
Lakini mshahara wa Poulsen unalipwa na Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo baada ya Rais Jakaya Kikwete kuagiza mishahara yote ya makocha wa timu za taifa ilipwe na serikali.
Watendaji wa wizara yenye dhamana ya michezo nchini hawakupatikana jana kuzungumzia suala hilo endapo serikali itakuwa tayari kulipa gharama hizo au mzigo huo utabaki kwa TFF.
Poulsen, aliyekuwa akizinoa timu za taifa za vijana, alisaini mkataba wa mwaka mmoja Mei 11, mwaka juzi kuinoa Stars akirithi mikoba ya kocha Jan Poulsen ambaye pia ni raia wa Denmark, mkataba uliomalizika Mei 15, mwaka jana kabla ya kusaini tena mpya wa miaka miwili ambao utamalizika Mei mwakani.
Wakati Malinzi akisita kueleza hatma ya Poulsen, tayari shirikisho hilo limeshaamua kuwatumia makocha wazawa katika mkakati wake wa kupata kikosi imara cha Stars kupitia michuano rasmi ya kitaifa itakayoanza Februari 22 hadi Machi 5, mwaka huu. Mikakati hii inafanywa bila kumshirikisha.
Kwa muda mrefu sasa baadhi ya wadau wa soka nchini wamekuwa wakiponda kiwango cha Stars, hasa katika kampeni za Kombe la Dunia zitakazopigwa nchini Brazil kuanzia Juni 12 hadi Julai 13.
Stars wakiwa katika Kundi C, Septemba mwaka jana waliishia hatua ya makundi baada ya kufanya vibaya katika mechi za marudiano na kumaliza nafasi ya tatu; nyuma ya Ivory Coast na Morocco huku Gambia wakiwa nafasi ya nne.

0 comments:

Chapisha Maoni