Kanali ya televisheni ya CNN imeuelezea mwaka 2013 kuwa ni mwaka
uliokuwa na mafanikio nadra kuwahi kushuhudiwa katika kadhia ya nyuklia
ya Iran. Kwa mujibu wa kanali hiyo, katika mwaka uliomalizika wa 2013
limetokea tukio katika uga wa kimataifa ambalo ni tofauti kabisa na
mazungumzo yote yaliyofanywa hapo kabla kati ya Iran na jamii ya
kimataifa, na kupatikana matunda katika mazungumzo hayo. Kinachoashiriwa
na CNN ni makubaliano ya Novemba 24 baina ya Iran na nchi sita
zinazojulikana kama kundi la 5+1, ambazo ni Marekani, Uingereza,
Ufaransa, China, Russia na Ujerumani; makubaliano ambayo yalifikiwa huko
Geneva baada ya takribani miaka kumi ya misuguano na propaganda dhidi
ya shughuli za nyuklia za Iran. Kwa mtazamo fulani, makubaliano hayo ni
azimio la kisiasa la mpango wa pamoja wa pande mbili unaokusudiwa
kutekelezwa kwa sura ya kujitolea ili kujenga hali ya kuaminiana katika
kadhia ya nyuklia na hatimaye kufikia kwenye lengo la pamoja.
Kwa mtazamo mwengine tunaweza pengine kusema kuwa katika kipindi
kipya cha urais hapa nchini yameshuhudiwa mabadiliko maalumu ambayo
natija yake ni makubaliano ya awali yaliyofikiwa Novemba 24 huko Geneva.
Bila ya shaka mabadiliko hayo yametokana na majimui ya tajiriba na
matukio yaliyojiri katika mazungumzo ya nyuklia ambayo yameyafanya
madola ya Magharibi yachukue msimamo unaozingatia uhalisia wa mambo
kutokana na hatua za Iran za kujenga hali ya kuaminiana katika suala la
nyuklia. Hata hivyo msimamo huo umechukuliwa kwa kuchelewa kwa muda wa
miaka kadhaa, kwa sababu viongozi wa juu kabisa wa Jamhuri ya Kiislamu
ya Iran walikwishatangaza mara kadha wa kadha kwamba taifa hili halina
nia ya kumiliki silaha za atomiki na kwamba kutokana na imani, itikadi
na thamani za kidini, silaha hizo hazina nafasi yoyote katika mfumo wake
wa ulinzi. Kinyume na vile unavyojaribu kuonyesha ulimwengu wa
Magharibi, sera za msingi na za utekelezaji za Iran zinasisitiza juu ya
kutekelezwa kikamilifu mkataba unaopiga marufuku uundaji na uenezaji
silaha za nyuklia NPT. Na kwa kweli makubaliano ya Iran na kundi la 5+1
katika kadhia ya nyuklia yamefuata muelekeo huo. Na ndiyo maana licha ya
kupokewa na kuungwa mkono na jamii ya kimataifa, makubaliano hayo
yameuchukiza mrengo maalumu unaojumuisha utawala wa Kizayuni wa Israel
ambao umekuwa ukificha ukweli kuhusu silaha zake za atomiki nyuma ya
pazia la zogo na propaganda dhidi ya shughuli za amani za nyuklia za
Iran. Katika kipindi chote cha miaka ya hivi karibuni, Israel, ambayo ni
mmiliki pekee wa silaha hatari za atomiki katika Mashariki ya Kati
imekuwa ikitumia kila fursa inayopata ikiwemo ya vikao vya Baraza Kuu la
Umoja wa Mataifa kujaribu kuuhadaa ulimwengu kwa kutoa taswira potofu
na ya kupindua ukweli kuhusu shughuli za nyuklia za Iran. Nukta nyengine
kuhusu sababu zilizochangia kupatikana mwafaka kati ya Iran na kundi la
5+1 ni kugonga mwamba madola ya Magharibi katika sera yao ya kuiwekea
Iran vikwazo vya kidhalimu na visivyo na uhalali wa kisheria. Kutokana
na tajiriba yaliyopata, madola hayo yametambua kwamba taifa la Iran
halitosalimu amri kwa sababu ya vikwazo, wala halitoyumbishwa na vitisho
vya Magharibi. Isitoshe ni kwamba zile nchi ambazo kwa muda wote huu
zimekuwa zikifuata mkumbo katika sera ya vikwazo inayotekelezwa na
Marekani hazina hamu tena ya kushabikia suala hilo linalozigharimu na
kuzipotezea mabilioni ya dola. Lakini nukta ya mwisho ni kwamba
makubaliano ya Geneva yalikuwa ushindi kwa wote na yalithibitisha kuwa,
kwa kufikia makubaliano ya pamoja na kwa kuheshimiana, inawezekana
kufikia kwenye ufumbuzi wa kimantiki. Pamoja na yote hayo makubaliano ya
Geneva ni hatua ya kwanza mbele kuelekea kwenye mwafaka kamili. Hatua
hiyo ilipigwa katika mwaka 2013, na ilivyokubaliwa, mnamo mwishoni mwa
mwezi huu wa Januari, itaanza awamu ya utekelezaji wa makubaliano hayo.
Ndiyo kusema kwamba bado kuna safari ndefu na ngumu hadi kufikia kwenye
mwafaka kamili




0 comments:
Chapisha Maoni